JK ataja gharama za daraja la Kigamboni
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, ametaja gharama za ujenzi wa daraja la Kigamboni, Dar es Salaam.

JK ameandika kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii, Facebook kuwa gharama za ujenzi wa daraja hilo ni shilingi bilioni 214.6.
Alisema, fedha hizo zitalipwa na serikali kwa asilimia 40 na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), litalipa asilimia 60 kugharamia mradi huo.
“Daraja Mradi: Ujenzi wa Daraja la Kigamboni. Gharama: Tshs. Bilioni 214.6+ (60%, 40%; NSSF, Serikali) Muda: Miezi 36,” alisema Kikwete.
Kutokana na ufafanuzi wa JK kuwa daraja hilo litakamilika ndani ya kipindi cha miezi 36, inaonesha kuwa litaanza kutumika kabla ya kumalizika kwa kipindi chake cha utawala.
Daraja hilo, linatarajiwa kuanza kujengwa Februari mwaka huu na kukamilika Februari 2015, wakati JK atamaliza muhula wake wa uongozi Novemba 2015.