Eti Diamond naye ni Freemason!
Yapo madai kwamba kwamba mwanamuziki Nasibu Abdu Juma ‘Diamond Platnumz’ ni memba wa jamii ya siri inayodaiwa kumwabudu shetani, Freemason.
Chanzo cha madai hayo ni picha iliyovuja mitandaoni, ikimuonesha Diamond na jamaa wa kizungu, anayedaiwa kuwa mfuasi mwenye cheo ndani ya Freemason.

Inaelezwa kuwa picha hiyo, Diamond alipiga na mzungu huyo, nchini Uingereza, alipokwenda kwenye ziara yake ya kimuziki.
MAVAZI
Ilidaiwa pia kuwa mavazi ya Diamond (meusi) yalishabihiana sawia na yale ya mtasha huyo yanayoelezwa kuwa sehemu ya mavazi ya jamii ya Freemason.
ISHARA
Kingine kilichoibua maswali ni ishara ya salamu ya wawili hao ambayo ilitengeneza nembo ya Freemason ya ‘V’ au bikari kwa namna walivyogusana kwa vidole.
Kwa mujibu wa wadau walioiona picha hiyo iliyonaswa kwenye mtandao wa Twitter, Diamond amekuwa na ishara nyingine nyingi za aina hiyo hivyo kuzidi kuzua utata kama ni memba wa jamii hiyo.
“Lakini inawezekana kwa sababu nasikia ukishajiunga unapata mafanikio ya ghafla. ‘So’ kuhusu hili, sina upande wa kusimamia,” ilisomeka sehemu ya maoni kwenye mtandao huo baada ya kuibuka mjadala mzito juu ya ishu hiyo inayozidi kushika kasi mithili ya moto wa kifuu.
“Tungeshukuru kama Diamond mwenyewe angejitokeza aseme ukweli kwani akinyamaza anazidi kutuweka njia panda,” ilisomeka sehemu nyingine ya maoni hayo huku ikiungwa mkono na wengi.
KAULI YA DIAMOND
Staa huyo wa Bongo Fleva alipoulizwa alijibu: “Nakumbuka walinifuata watasha wengi tofauti lakini huyo mmoja alining’ang’ania sana nipige naye picha.
“Kwa kweli alinilazimisha sana kwa sababu mwanzo nilikataa lakini baadaye nikaona isiwe ishu nikampa ushirikiano alioutaka. Mimi sikuona matatizo alivyotaka tusalimiane kwa kugusisha vidole kwa sababu nilikuwa sijui chochote kuhusu Freemason. Nimeijua baada ya mambo haya kuyasikia kwa sana hivi karibuni.
“Kwa hiyo inawezekana siku hiyo waliniunganisha bila mimi kujua (kicheko).”
SASA UKWELI NI UPI?
Mara kadhaa Diamond amekuwa akihusishwa na Freemason kutokana na mafanikio ya ghafla aliyoyapata na mvuto alionao kwa mashabiki wake ndani na nje ya Bongo, lakini yeye anafafanua hivi:
“Si kweli bwana, mimi nazisikia tu hizi habari kama wengine. Nasikia tu ipo hapa Bongo na kiongozi wake ni Sir Andy Chande, zaidi ya hapo sijui chochote.
“Mimi ni mtu wa swala tano na mafanikio yangu naamini Mungu ndiyo kila kitu.”