Music | Lifestyle+Fashion | Antivirus | Love+Relationships | Business+Politics | Sport | TUMA Registrations

You are here:   HomeMusic
| + -

Music

Tuesday, 21 May 2013 11:12 Al News - Music
Print PDF

Kuhusu Tuddd Thomas na Tuzo za Kili

Mashabiki wa mtayarishaji wa muziki (Producer), mwenye uwezo wa kipekee, aliyetayarisha wimbo wa Leka dutigite wa Kigoma All Stars na zingine nyingi, Tudd Thomas, wamekuwa wakiulizana maswali mengi wao kwa wao pasipo kupata majibu.

Safari ya Tudd Thomas katika muziki, ilianzia mkoani Iringa akiwa Iringa Records aliporekodi wimbo wa mwanamuziki Marlaw unaoitwa Bembeleza. Wimbo huo ulipata tuzo ya wimbo bora wa mwaka kutoka Kilimanjaro Tanzania Music Awards mwaka 2008 na pia kumfanya Marlaw apate tuzo ya msanii bora wa kiume kupitia tuzo hizo. Baadae alihamia jijini Dar es Salaam na ndipo alipoonesha uwezo wake zaidi kwa kusuka nyimbo zilizotikisa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla.

Hakuna asiyeufahamu wimbo wa Pii Pii (Missing my baby) wa Marlaw ambao aliutengeneza yeye kupitia Studio ya JML. Wimbo huo ulipata tuzo nyingi ikiwa ni pamoja na tuzo ya Nzumari nchini Kenya mwaka 2009 mbapo uliingia kwenye kipengere cha wimbo bora wa Afrika Mashariki, kumfanya Marlaw aingie kwenye kipengele cha msanii bora wa Afrika Mashariki na kunyakua tuzo hiyo. Baada ya hapo wimbo huo ulipata tuzo ya Kilimanjaro nchini Tanzania kama wimbo bora wa mwaka wa Afro pop mwaka 2010, tuzo ya Chaguo la Teneez Music nchini Kenya kama wimbo ulioongoza kwa kuchukuliwa kwa njia ya mtandao Afrika Mashariki “The most downloaded East African song” mwaka 2010, pamoja na tuzo ya Nigeria Sound City Video Music kama wimbo bora wa Afrika Mashariki mwaka 2010.

Aliendelea kutayarisha nyimbo ambazo zilipata umaarufu mkubwa na kuingia kwenye vipengele mbalimbali vya tuzo za muziki za Kilimanjaro. Mwaka 2012, nyimbo tatu zilizotokana na mikono yake zilipata nafasi ya kushiriki tuzo hizo. Nyimbo hizo ni Liz One wa Izzo Business ambao uliingia kwenye vipengele viwili ambavyo ni wimbo bora wa mwaka na wimbo bora wa Hip hop na pia kusababisha msanii huyo aingie kwenye kipengele cha msanii bora wa Hip hop. Milele daima wa Barnaba na Kizunguzungu wa Rachel, ambapo zote ziliingia kipengele cha wimbo bora wa Zouk/Rhumba pia ni nyimbo alizotengeneza mtayarishaji huyo.

Nyimbo zingine alizotayarisha ambazo zilifanya vizuri kwenye vituo mbalimbali vya redio na TV ni Kisa pombe na Soldier za Mwasiti, Sorry sana, Mbayuwayu na Mtoto wa Afrika za Marlaw pamoja na Natumaini ya Becka aliyowashirikisha Barnaba na Amin. Pia zipo nyingine kama Unikimbie ya Amin, Tushukuru kwa yote ya Ditto, Lonely ya Linah na Magubegube ya Barnaba.

Mtayarishaji huyo ambaye hajawai kuingia kwenye tuzo za Kilimanjaro za muziki wa hapa nchini Tanzania ambazo mwaka huu zimeongezewa kipengele cha Mtayarishaji bora chipukizi ndiye aliyetayarisha wimbo wa Leka dutigite wa Kigoma All Stars kupitia Studio yake ya Ngoma Records. Wimbo huu umeingia kwenye kipengele cha wimbo bora wa mwaka 2013. Pia alishirikiana na mtayarishaji Imma the boy kutengeneza wimbo wa Me ‘n’ U wa Ommy Dimpoz ambao umeingia kwenye kipengele hicho na vipengele vingine ambavyo ni wimbo bora wa Bongo Pop na wimbo bora wa kushirikiana.

Alipoulizwa alisema hapendi kuzungumzia juu ya kutotajwa kama miongoni mwa wanaowania tuzo. Aliendelea kusema kwamba, hata kama baadae ikitokea, kwake ni motisha tu, lakini kikubwa zaidi ni kwamba anahisi analo deni kubwa la kutumia uwezo wake ipasavyo kufanya kazi nzuri zaidi ya hapo ili kuutangaza muziki wa Tanzania kimataifa. Pia alisema ana malengo makubwa aliyojiwekea na ndiyo maana kila kukicha anawaza kutayarisha nyimbo zenye tofauti na zenye radha ya kipekee.

Tudd Thomas anaendelea kukitumia kipaji chake na ujuzi wake ipasavyo na siku chache zilizopita kuna nyimbo zisizopungua tatu zilizoingia sokoni na zinafanya vizuri, ambazo ni kazi za mikono yake. Nyimbo hizo ni Uswazi take away ya Chegge, Nyumbani ya Kigoma All Stars na pia ameshirikiana kwa kiasi kikubwa na mtayarishaji Fundi Samwel kutengeneza wimbo wa Mahakama ya mapenzi wa Linex.

 
Monday, 13 May 2013 00:00 Al News - Music
Print PDF

Ruge, Kusaga wakimbilia mahakamani, wamshatki Jide

Staa wa Bongo Fleva, Judith Wambura 'Lady Jaydee', leo alifika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, kufuatia kufunguliwa kesi ya madai katika mahakama hiyo.

Katika hati ya madai hayo, mwanamuziki huyo anashtakiwa na viongozi wa Clouds Media Group ambao ni Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga.

Tuhuma za kesi hiyo zinatarajiwa kusomwa mahakamani hapo na Hakimu, Athuman Nyamrani Mei 27 mwaka huu.

Jaydee aliwasili mahakamani hapo akiwa na mumewe, Gadner G. Habash, mishale ya saa 6 mchana na kuongoza moja kwa moja chumba cha makarani wa mahakama hiyo ambao aliwakabidhi hati ya mashitaka hayo.

Awali, ilielezwa kuwa Jide leo angefikishwa Mahakama ya Kinondoni, Dar bila kutajwa aina ya mashitaka yanayomkabili.

Taarifa za mwanadada huyo kufikishwa mahakamani hapo, ziliibuka chinichini kwenye mitandao ya kijamii, mwishoni mwa wiki iliyopita ambapo baadaye Lady Jaydee alihoji kuwa pengine yeye ndiye anayestahili ‘kukinukisha’ kwa kuwapeleka mahakamani wasanii walio chini ya Tanzania House of Talent (THT), Estalina Sanga ‘Linah’ na Elias Barnaba.

Jide alisema kuwa aliwalipa Lina na Barnaba kianzio cha shoo yake ya Mei 31, mwaka huu kisha kumchomolea dakika za mwisho.

“Hivi mahakamani sitakiwi kwenda mimi ambaye wasanii wao wamechukua advance na kuafiki mbele ya camera na wakanipa, It wasn’t me?” aliandika Lady Jaydee katika mtandao wa Twitter.

KUMBUKUMBU

Kumbukumbu inaonesha, miongoni mwa maneno ambayo yanadaiwa kuwa yaliuchafua uongozi wa Clouds ni yale ambayo Lady Jaydee aliyaandika kupitia blogu yake hivi karibuni, akitoa waraka aliouita wosia kwa Rugen a Kusaga ikitokea yeye akitangulia kufa kabla yao.

Katika wosia huo, Jise alisema kuwa Rugen a Kusaga ni watu wabaya, wanaomuua kimuziki, akatamka kwamba siku akifa redio yao isipige nyimbo zake wala kutoa ripoti yoyote ya msiba, wao wenyewe wasisogee kumzika na watu wakitokea, watakaokuwepo wawapige mawe.

RUGE HAKUKAA KIMYA

Hata hivyo, siku chache baada ya Lady Jaydee kuandika wosia huo mzito, Mkurugenzi wa Vipindi na Utafiti wa Clouds Media Group, Ruge Mutahaba alitumia Kipindi cha Power Breakfast kuzipangua hoja moja baada ya nyingine na mwishoni kumalizia kwa kusema Jide anapaswa kusoma alama za nyakati kwani umri unakwenda na muziki anapaswa kujipanga vizuri ili uweze kujimudu pindi zamu ya kushuka kwenye gemu inapofika.

Kuhusu wito wa mahakamani, Jide ‘ali-tweet’: “Nimepata taarifa zisizo rasmi kuwa nimefunguliwa kesi mahakamani, natumaini sitaitwa kizimbani tar. 31 May ambayo ndiyo siku ya show.”

Baadaye aliongeza: “Ratiba ya usiku wa leo (Ijumaa iliyopita) ni Machozi Band kama kawaida, ila ratiba ya Jumatatu (leo) natakiwa Mahakama ya Kinondoni. Taarifa zaidi zitafuata nikijua kinachoendelea. Ila kwa leo mje tuburudike Nyumbani Lounge mpaka asubuhi.”

 
Friday, 03 May 2013 07:27 Al News - Music
Print PDF

Mashambulizi ya Jaydee kwa Ruge, Kusaga yaibua msukosuko

Mwanamuziki mkongwe wa Bongo Fleva, Judith Wambura ‘Lady Jaydee’ ameendelea kuwakaba koo wakurugenzi wa Redio Clouds FM, Joseph Kusaga na Ruge Mutahaba.

Jide, ameibua msukosuko wa aina yake nchini kufuatia tamko lake alilotoa jana, akibainisha kwamba Kusaga na Ruge si watu wema na hata akifa, redio yao isitangaze kifo chake wala kupiga nyimbo zake, vilevile na wao hawatakiwi kuhudhuria.

Hili ndiyo tamko lenyewe…

WOSIA WANGU KAMA IKITOKEA NIMETANGULIA KUFA KABLA YA RUGE AU JOE KUSAGA

Watu wanashtuka mtu akiongelea kifo, Utafikiri hawafahamu fika kuwa kila nafsi itakionja, Kwenye maisha yangu nimepitia mambo mengi, magumu na mepesi na bado naendelea ku-experience mambo magumu zaidi kadri ninavyozidi kuwa mkubwa.

Siku za karibuni nimekuwa nikipigwa vita sana na watu wenye uwezo mkubwa kifedha , ki umri na hata wenye ukubwa wa connection katika hii industry ya muziki. Wanaomiliki chombo cha habari.

Nasimama na kusema kuwa sitokata tamaa, kwani lengo lao kubwa ni kuona na kuhakikisha nimeanguka kabisa na sipo katika ramani ya muziki.

Watu hao ambao vita yao ilikuwa baridi miaka kumi iliopita, sasa inazidi kuwa moto baada ya kutambua kuwa mimi ni mtu mwenye maamuzi yangu na misimamo yangu bila kuburuzwa.

Wanapita kila mahali kuhakikisha kila mrija unaoniingizia chochote unakatika, na hiyo ni kutaka kuuthibitishia umma wa Tanzania kuwa hakuna msanii anaeweza ku survive bila wao. Mimi ni msanii tofauti na hao mnaofikiria.

Nadhani mnafahamu tangu niachane na Tuzo zenu mnazo influence nani apate nani asipate, na tangu niachane na Fiesta nilipolipwa laki 8 mara ya mwisho na kuamua kuunda Band ili nijiajiri na kupata shows zangu mwenyewe, ikafanikiwa sana jambo ambalo limewauma na kuamua kufanya kitu cha kuiangusha Band yangu. Nita survive kwa njia zozote MUNGU alizonipangia.

Wakati bado wote tunapumua na kwakuwa watu hao hawanipendi kabisa, Naamini fika hawataweza kunipenda hata siku nitakapokuwa nimekufa. Na huu ndio wosia wangu kwa watu hao.

Natambua wanaweza kutumia redio yao kutangaza sana kifo changu na kusema marehemu alikuwa mtu mzuri na pengine kupiga nyimbo zangu kuanzia asubuhi mpaka jioni.

Ila naomba nitamke hivi, siku nikifa CLOUDS FM isipige nyimbo zangu, wala isiongelee lolote kuhusiana na kifo changu. Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga wasihudhurie msiba wangu, na mkiwaona muwapige mawa enyi mtakaokuwa hai baada yangu.

Kama wamenifitini, na hawajanipenda nikiwa hai hakuna haja ya kujifanya kunipenda nikiwa marehemu. Sina haja wanipende pia kwakuwa mimi sio ndugu yao, Ila ubaya wanaoundeleza mioyoni mwao wanaujua na nina hakika nafsi zao zinawasuta pia.

Niliamua kujiepusha nao miaka mingi na kufanya biashara zangu, nimekaa kimya watu wanafikiri nabebwa lakini sijabebwa chochote sikutaka ugomvi haya mambo yalianza baada ya Album yangu ya pili ya Binti mwaka 2003 nilipojitoa Smooth Vibes chini ya Ruge.

Nilivumilia fitna nikiamini ipo siku yatakwisha lakini naona moto ndio unazidi kuwaka. Na hii ni kwasababu wanaogopa msanii akiwa mkubwa watashindwa kumuamrisha, Hamuwezi kumiliki dunia..

Kama mnasema mlinibeba mbona hamkuwabeba dada zenu wa tumbo moja waimbe ili hela irudi nyumbani??. kama kweli wewe Kusaga unajua kubeba basi beba jiwe liimbe liwe star..

Kwa roho zenu mbaya mnaweza kumbeba mpita njia nyie? Talent haibebwi, hujibeba kama mnabisha si mna watoto wabebeni basi wawe kama kina Diamond ndio nitaamini kweli nyie mnaweza kubeba watu.

Mnawatishia wasanii kuwa yoyote atakaefanya nyimbo na mimi hazitapigwa, vikao vinne mmeshakaa kunijadili. Mnadhani je! nitapungukiwa nini endapo wasanii wengine wakiacha kufanya kazi na mimi?? nyimbo hazitakuwa nzuri.

Basi sawa ngoja tuone MUNGU ni nani, Binadamu nani? Kwahiyo mtaamrisha watu pia wasikae na mimi? Ilikuwa niseme majina matatu huyo mmoja nimemsamehe baada ya kugundua sio hiyari yake ila yuko under influence ya hawa jamaa wawili.

Kila siku mnamsingizia Ruge peke yake Kusaga ni mfitini kuliko hata huyo Ruge, watu hamjui tu.

Mtu hela zote hizo bado shillingi mbili ya Jide inakuuma? Roho gani hiyo??

Naishia hapo na sitabatilisha kauli yangu

 

 
Wednesday, 24 April 2013 19:47 Al News - Music
Print PDF

Jina la Biggie latumika kunadi mjengo

Mjengo wa kifahari uliopo eneo la Clinton Hill, Brooklyn, New York, Marekani, unauzwa kwa thamani ya dola za 750,000, sawa na shilingi 1.2.

Mchawi wa Freestyle, Christopher Wallace ‘Notorious B.I.G’, aliishi kwenye mjengo huo wakati akiwa mdogo.

Kwa vile B.I.G a.k.a Biggie aliishi hapo enzi hizo, wamiliki wa jengo hilo, wameamua kutumia jina lake kwa ajili ya kulinadi, kwa imani kwamba litapata wateja kwa urahisi.

Matangazo mengi mtandaoni, yanasomeka: “Nyumba aliyoishi Biggie inauzwa.”

Familia ya Biggie ambaye alifariki dunia miaka 16 iliyopita, haijatoa tamko kama inaona sawa au kuchukizwa na matumizi ya jina la mkali huyo wa Hip Hop katika mauzo ya mnada wa jengo hilo.

 
Tuesday, 23 April 2013 14:22 Al News - Music
Print PDF

Lady Jaydee: Mungu si Ruge wala Kusaga

Stadi wa Bongo Fleva, Judith Wambura ‘Lady Jaydee’ ametamka kwamba anaamini hatarudi nyuma na hatatetereka kimuziki kwa sababu anamtumaini Mungu.

Kupitia akaunti yake ya mtandao wa kijamii ya Twitter, Jaydee a.k.a Binti Komando, aliandika: ‘Mungu siyo Ruge wa Kusaga kwa hiyo naamini nitashinda.”

Kabla ya hapo, Jaydee ak.a Jide ambaye zamani alipenda ajulikane kama Binti Machozi, aliandika: “Msemo wa Mungu siyo Athumani kila mtu anaujua, ila mimi ninao mpya.”

Baada ya muda mfupi ndipo akaandika: “Msemo wangu naamini Mungu siyo Ruge wala Kusaga, kwa hiyo naamini nitashinda.”

Jide ambaye ni mmoja wa wanamuziki waasisi wa Bongo Fleva, ameamua kujiweka wazi kiharakati, akipingana na unyonyaji wambao unafanywa katika muziki na washikadau.

Jide kama ambavyo kaka zake wa Vinega walivyokuwa wanafanya katika mixtape za Anti Virus, anawashambulia wakurugenzi wa Clouds Media Group, Joseph Kusaga na Ruge Mutahaba pamoja na kituo chao cha redio cha Clouds FM.

 
Thursday, 18 April 2013 06:41 Al News - Music
Print PDF

Kweli Bi. Kidude ametutoka

Mwanamuziki mkongwe wa Taarab, Fatuma Binti Baraka Khamis,  maarufu kwa jina la  Bi Kidude amefariki dunia leo huko Bububu Zanzibar, sehemu alikokuwa anauguzwa.

Taarifa hizo, zinafuatia uvumi wa mara kwa mara kwamba Bi. Kidude hatunaye lakini nyakati zote zilikuwa uzushi ila sasa ni ukweli kwamba mkongwe huyo ametutoka.

Habari zinasema kuwa, mwili wa marehemu Bi. Kidude, utahamishiwa nyumbani kwake Rahaleo na mazishi yanatarajiwa kufanyika kesho.

Sababu ya kifo chake haijawekwa wazi lakini ukweli ni kwamba Bi. Kidude alikuwa anasumbuliwa na maradhi ya kisukari kwa muda mrefu na tangu mwaka jana, hali yake ilikuwa tete sana.

Vilevile, zipo taarifa kwamba Bi. Kidude alikuwa anasumbuliwa na maradhi ya uvimbe kwenye kongosho.

Bi Kidude alizaliwa katika kijiji cha Mfagimaringo, alikuwa binti wa mchuuzi wa nazi, hakuna anayejua haswa Bibi huyu alizaliwa tarehe ngapi, wapo wengine wanaoamini kwamba mpaka mauti yamemfika, kulikuwa na uwezekano alishafikisha zaidi ya umri wa miaka 102.

Katika mwaka 1920 tayari alikuwa amekwisha anza kuimba katika vikundi vya sanaa kule kwao, mwaka 1930 alijiunga na Egyptian Musical Club ya Dar es Salaam na kuzunguka miji mingi ya Tanzabua Bara, mwaka 1940 alirudi Zanzibar ambako awali alikuwa amekimbia kwa kuwa aliozwa kwa nguvu na mtu aliyemzidi sana umri.

Bi Kidude pia aliwahi kuimba na Sitti Binti Saadi wakati wa ujana wake  na katika maisha yake Bi Kidude amekwisha zunguka mabara yote akiimba katika majukwaa na wanamuziki maarufu ulimwenguni.

Na kuhusu kuzaa, haijawahi kuripotiwa popote kama Bi. Kidude aliwahi kuzaa.

Mungu Amlaze Pema Peponi Bibi yetu. Amen.

 
Thursday, 18 April 2013 06:04 Al News - Music
Print PDF

Bosi wa East Africa Melody afariki dunia

Mkurugenzi wa Kikundi cha Taarab cha East African Melody, Hadji Mohamed, amefariki dunia asubuhi hii baada ya kuugua kwa muda mfupi katika hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Taarifa zaidi kuhusu kifo hicho, zitakuja baadaye.

 
Tuesday, 02 April 2013 21:19 Al News - Music
Print PDF

Roma siyo mwana Hip Hop, anaimba ngonjera

Rapa Ibrahim Mussa Mshamu ‘Roma Mkatoliki’, amepoteza dira, maringo yanammeza, anagombana mpaka na watu waliomsaidia kufika mahali alipo.

Hazijapita siku nyingi, tangu Roma alipodaiwa ‘kuwadisi’ watangazaji, wakati akiwa jukwaani, akifanya shoo ya kuwasindikiza Kigoma All Stars ‘Leka Dutigite’, Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Wiki mbili zilizopita, gazeti ndugu na hili la Ijumaa Wikienda, kupitia safu yake ya Kiti cha Moto, lilichapisha maoni ya wasomaji ambao wengi wao walimkosoa Roma kwa tabia yake ya maringo na kuwadharau watu.

Ni Roma huyohuyo, katika tamasha lililoandaliwa na kampuni moja ya simu za mkononi mapema mwaka huu, Coco Beach, Dar es Salaam, alichelewa kufika eneo la tukio, hivyo kusababisha usumbufu mkubwa.

Mashabiki walirusha chupa na mawe jukwaani, amani ikahatarishwa, chanzo kikiwa ni mtu ambaye amelipwa fedha kwa ajili ya kazi yake, akapangiwa muda lakini kwa makusudi akachelewa.

Mbaya zaidi ni kwamba katika wanamuziki wote walioalikwa kutumbuiza kwenye onesho hilo, ni Roma peke yake aliyechelewa.

Mashabiki wakawa wanauliza alipo Roma kwa sababu walitangaziwa atakuwepo, mwisho wakafanya fujo kwa imani kwamba wametapeliwa. Kumbe rapa mwenyewe ndiye tapeli wa muda.

UNAONA ALIVYO KIMEO?

Kama tabia yake inawachukiza mashabiki kwa kiwango ambacho mpaka wao wenyewe wanatuma maoni kumkosoa kwamba ana maringo, kiburi na dharau, hapo anachezea shilingi kwenye choo cha shimo.

Umaarufu na mafanikio ya Roma, havijafikia hata theluthi moja ya Nice Lucas Mkenda ‘Mr. Nice’ lakini leo hii yupo wapi? Dharau, nyodo, kiburi na maringo, viliwachukiza mashabiki, wakamtema, leo anahangaika.

Kama Nice anatumikia adhabu ya kile alichowafanyia mashabiki miaka ya nyuma, Roma yeye ni nani mpaka yasimkute? Kila mtu huvuna alichopanda. Siku zinavyozidi kwenda, atajikuta hana mpya.

Kivipi anawadisi Watangazaji? Bila watu hao Roma siyo lolote. Ni utovu wa busara, kuingia mgogoro na wanaoufanya muziki wake usikike. Kwa vile hajitambui, kweli ni kimeo!

Kwa matukio mithili ya lile la Coco Beach, sasa siwezi kushangaa ni kwa nini Roma hapati shoo nyingi. Mapromota wanamwogopa, pale alipo anajiona ameshakuwa Shawn Cutter ‘Jay Z’, wakati kiwango chake bado kipo chini sana.

Sasa atakimbilia wapi ikiwa kila upande sasa anaonekana kimeo? Roma anatakiwa kutambua kuwa kipaji ni kipengele kimoja lakini mvuto wa kibiashara anatakiwa aujenge yeye mwenyewe.

WANA HIP HOP HAWAMKUBALI

Mwaka jana, alizua gogoro zito kwa wadau wa Hip Hop, pale alipopewa tuzo mbili za Mwanamuziki Bora wa Hip Hop na Wimbo Bora wa Hip Hop kupitia singo yake ya Mathematics.

Wadau wa Hip Hop, walikosoa kwamba Tuzo za Kili (Kilimanjaro Tanzania Music Awards), zilikosa weledi kwa kumpa tuzo Roma kwa sababu hana vigezo.

Prodyuza mkongwe nchini, Paul Matthysse ‘P. Funk’, alisema: “Yule siyo mwana Hip Hop, ndani ya Roma hakuna Hip Hop, yule ni mpiga kelele tu.”

Hili la Roma kuwa mpiga kelele, limekuwa likisemwa na wengi kwamba hushindwa kuzingatia aina ya nyimbo, badala yake hupayuka kiasi ambacho humfanya msikilizaji asijue anachorap.

HAJUI KUTUNGA

Kingine ambacho Roma anatakiwa kujirekebisha ni kujifunza kutunga, kwani nyimbo zake hazioneshi uwezo wake wa kuandika, bali kile ambacho hufanya huwa ni kugusa vitu mbalimbali.

“Huwa haoneshi uwezo wa kisanii, ndani ya mstari mmoja anaweza kugusua vitu viwili au vitatu bila kutoa picha rahisi kwa msikilizaji. Hii huwafanya wengi ambao wanakuwa hawajui vitu anavyorap, wabaki gizani, huo siyo usanii.

“Utunzi huendana na hoja. Angalia nyimbo za akina Profesa Jay (Joseph Haule) au MwanaFA (Hamis Mwinjuma), wakiimba kitu wanasaidia msikilizaji aelewe vitu kwa uchambuzi wa hoja za kisanii.

“Watu wanaoweza kumshabikia Roma, labda ni wale wapenda kelele ila wanaojua muziki lazima watofautiane naye,” alisema mwana Hip Hop mwenye heshima kubwa nchini kwa sharti la kutotajwa jina.

Mwana Hip Hop huyo akaongeza: “Hip Hop ni hoja, angalia hata mashairi ya Fid Q (Fareed Kubanda). Roma siro rapa, ni mwimba ngonjera. Hata tungo zake zimekaa kingonjerangonjera. Kimahesabu, yeye ndiye rapa Bongo mwenye tungo dhaifu zaidi.”

ANAYO NAFASI YA KUJIREKEBISHA

Mtu anapokosolewa, inabidi kujisahihisha ili kuishi ndani ya mstari unaokubalika. Pamoja na yote ambayo anakosolewa, binafsi naamini anaweza kujirekebisha na kufanya vizuri.

Kama ni maringo, kiburi, jeuri na dharau, basi aache. Kuhusu uzingatiaji wa muda anapopewa kazi ya kutumbuiza, inafaa aheshimu, kwani hiyo ni ajira yake. Namshauri asipotee kwa kuendekeza kuwadisi watangazaji.

Kuhusu tungo, ule ni ushauri tu, bila shaka akiwaona akina Prof. Jay, FA, Fid Q na wengineo, wanaweza kumfunda namna bora ya kuandika mistari iliyoshiba hoja za kisanii ili aachane na mashairi ya ngonjera kama mwana Hip Hop mwenzake alivyomkosoa.

Makala haya ni maoni ya ripota wa DeiwakaWorld, siyo msimamo wa Deiwaka.

 
Tuesday, 02 April 2013 20:56 Al News - Music
Print PDF

Rihanna achekelea picha za X

Robyn Rihanna Fenty, wikiendi iliyopita alikosolewa sana baada ya kuingiza picha za X kwenye akaunti yake ya mtandao wa Instagram.

Rihanna ambaye wiki iliyopita, uliibuka uvumi kuwa amemwagana na mchumba wake, Chris Brown, siyo tu kwamba aliweka picha za X, bali pia alichekelea.

Mwanamuziki huyo, aliweka picha za wacheza shoo wakiwa wamevua nguo na kubaki uchi kwa sehemu kubwa ya miili yao kisha akaandika: “Naipenda sana kazi yangu.”

Akaendelea kuandika kwenye picha hizo: “Kwa kazi yangu, napata fedha nyingi.”

Kitendo hicho, kimesababisha akosolewe sana, huku wakosoaji wakisema amekosa maadili na amejishusha.

 
Monday, 01 April 2013 14:56 Al News - Music
Print PDF

Mke wa mtu apewa kipigo, kisa demu

Mke wa mtu ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja, juzikati alipatwa na aibu nzito baada ya kupandwa na midadi na kumvaa mwanamuziki Nasib Abdul ‘Diamond’ jukwaani kisha kumfanyia vituko.

Tukio hilo lilijiri kwenye ukumbi mmoja uliopo Kahama ambapo Diamond na kundi lake walikwenda kufanya shoo.

Kikianika ishu ilivyokuwa, chanzo chetu kilifunguka: “Wakati Diamond akidondosha wimbo mmoja baada ya mwingine, watu wengi walionekana kuchizika ile mbaya.

“Mwanamke mmoja mke wa mtu aliyekuwa amefika pale na jamaa yake, mzuka ulipomzidia, alipanda jukwaani kisha akaanza kumfanyia vituko Diamond.

“Alianza kumpapasa kimahaba na kama hiyo haitoshi, akaamua kumlamba kifua jamaa, unaambiwa ilikuwa ‘full’ balaa.”

Vituko vya mwanamke huyo jukwaani vilimfanya Diamond aonekane kuchizika ila baada ya mwanamke huyo kushuka jukwaani alipokelewa kwa kipigo na mumewe ambaye alionesha kukasirishwa na kitendo hicho.

Kutokana na kipigo alichokuwa akipewa mke wa mtu huyo, baadhi ya wasamaria wema waliamua kuingilia kati na kumuokoa ambapo ‘bishosti’ huyo aliondoka eneo hilo akilia.

 
Tuesday, 26 March 2013 03:50 Al News - Music
Print PDF

Isha Mashauzi: Mirungi, pombe inanisaidia jukwaani

Nyota wa muziki wa Taarab na mkurugenzi wa Mashauzi Classic, Aisha Ramadhan ‘Isha Mashauzi’ ameibua gumzo na kushangaza mashabiki baada ya kukiri kuwa yeye ni mtumiaji wa pombe kali na madawa ya kulevya aina ya mirungi.

Ishu hiyo ilijiri Alhamisi ya wiki iliyopita wakati akihojiwa na mtangazaji wa Redio Times FM, Hadija Shaibu ‘Dida’ kupitia kipindi chake cha Mitikisiko ya Pwani ambapo alisema mirungi na pombe kali ndiyo starehe yake kwani inampa stimu kabla hajapanda jukwaani na katika maisha yake ya kawaida nje ya usanii.

Mashauzi alifunguka hayo baada ya Dida kumtaka atoe ufafanuzi juu ya skendo ya kuvuta bangi inayomkabili ambapo alisema siyo kweli kwamba anavuta bangi ila akakiri kuwa anakula sana mirungi na kugida ulabu. Aliongeza kwamba kwa kuwa hana mume, mtoto wala hataki kuwa na familia, mirungi na pombe ndiyo vitu vinavyompa furaha maishani mwake.

Ripota wetu alipomtafuta Mashauzi ili kuipata ishu hiyo kiundani, alijibu kuwa hayo ni maisha yake hivyo kama anatumia mihadarati asifuatwefuatwe kwani ndiyo aina ya maisha aliyoyachagua.

 
Friday, 22 March 2013 06:31 Al News - Music
Print PDF

Prezzo kugonga shoo classic Aprili ndani ya Dar

Msanii kutoka 254 CMB Prezzo, anatarajia kufanya makamuzi ndani ya New Maisha Club - Dar es Salaam. Show hiyo inatarajia kufanyika ijumaa tar. 5 April 2013.

Prezzo atakuwa pamoja na wasanii wa hapa nyumbani watakao panda nae stage moja akiwemo Feza, Stereo, Shosteez na wengine surprise kwa mashabaki wa muziki wa kizazi kipya.

Hii ni mara ya kwanza kwa Prezzo kukamua ndani ya Club.

Prezzo ni msanii ambaye anafanya vizuri katika game, ladha fresh za single zake 2 mpya alizoziachia hivi karibuni akiwa moja ame - dedicate kwa marehemu mchumba wake Goldie ambayo inaitwa "Naija Girl". na nyingine ni Liqher ambao imekuwa gumzo Afrika Mashariki na Kati, zitasikika kwa mara ya kwanza live siku hiyo

Prezzo siku hadi siku anajizolea umaarufu mkubwa sana bara la Afrika hasa baada ya ushiriki wake katika jumba la Big Brother Star Game 2012 na kuibuka kinara namba 2 na kutuwakilisha Afrika Mashariki.Msanii ambaye amekuwa gumzo na stori kwa mashabiki mbalimbali ambaye juu ya muonekano wake kuwa wa kipekee (swagga) . Na siku zote amekuwa mtu wa watu.

Prezzo amefanya kazi kwa kushirikiana na wasanii mbalimbali akiwemo AY kutoka Tanzania, Wyre, Bamboo, Naziz na wengine kibao. Na nyimbo zake kushika chat katika vyombo mbalimbali vya habari,nyimbo kama Ma Fans, Naleta Action, Ma City Ma Town, Tupendane, For Sure For Shizzle na nyinginezo.

 

 
Tuesday, 19 March 2013 16:05 Al News - Music
Print PDF

Linex kuzindua Mahakama ya Mapenzi Maisha Club

Mjeda wa Bongo Fleva, mwenye sauti ya Kiafrika, Sunday Mangu ‘Linex’, anatarajia kuzindua ngoma yake mpya inayokwenda kwa jina la Mahakama ya Mapenzi.

Linex, atazindua ngoma hiyo mpya ndani ya Klabu ya New Maisha, Jumapili inayokuja (Machi 24).

Akipiga stori na ripota wetu, Linex alisema kuwa amejiandaa kufanya mapinduzi makubwa katika muziki wa Bongo Fleva, ndiyo maana amehakikisha anafanya shoo hiyo ya kiwango cha juu.

“Ni tathmini, nina mashabiki wengi, kwa hiyo lazima niwatumie kufanya mambo makubwa mwaka huu. Kwa kifupi mwaka huu na mingine inayokuja, nitaitumia ipasavyo kuitendea haki thamani yangu niliyonayo katika huu muziki,” alisema Linex.

Akaongeza: “Kuhusu nini ambacho nimedhamiria kukifanya siku hiyo pale Maisha Club, vilevile kuhusu mapinduzi ambayo nataka kuyafanya, vyote kwa pamoja ni wewe kuhakikisha unafika Maisha Club. Nawasihi mashabiki wa Mjeda Voice of Africa, waje tufanye yetu Jumapili.”

Kwa upande mwingine, Linex alisema kuwa ameiboresha familia yake ya Voices of Africa kwa kumchukua mwanadada mkongwe wa muziki wa Zouk nchini, Stara Thomas.

“Huo ni uhakika kabisa, Stara yupo Voices of Africa. Nitakuwa naye siku hiyo, kwa hiyo mashabiki wake pia watapata fursa ya kumuona kwa mara kwanza baada ya kuwa kimya kwa muda mrefu sana,” alisema.

 
Monday, 18 March 2013 15:19 Al News - Music
Print PDF

Shilole: Ziara ya muziki ‘Sauz’ imenisaidia sana

Baada ya kupiga shoo pande za Afrika Kusini, mrembo anayekomaa katika anga la muziki wa mduara Bongo, Zuwena Mohamed ‘Shilole’, amesema kuwa amejifunza mambo mengi kupitia ziara hiyo.

Shilole alisema, kwanza amejitambua na kupata mbinu mpya za kuhimili jukwaa hata kwa watu wasioelewa lugha unayoimba, mbinu mbalimbali za kujitangaza na ushirikiano.

“Nimejifunza mambo mengi, muziki una nguvu kubwa watu wanakuelewa kama una mbinu za kuwashawishi unapokuwa jukwaani, mashabiki wangu waendelee kunipa sapoti kwani mambo ndiyo kwanza yameanza,” alisema Shilole.

 
Wednesday, 06 March 2013 07:08 Al News - Music
Print PDF

Polisi wamfuatilia Ray C kila anapokwenda

Ili kuhakikisha harudi tena kwenye matumizi ya madawa ya kulevya, jeshi la polisi nchini, limemweka kati mwanamuziki Rehema Yusuf Chalamila ‘Ray C’.

Kamanda wa jeshi la polisi, kitengo cha kudhibiti madawa ya kulevya nchini, Godfrey Nzowa, amesema kuwa Ray C kila anapotembea anakuwa katikati askari wanaofuatilia nyendo zake.

“Kila anapokwenda, askari wamemzunguka. Tangu alipopata nafuu, tumekuwa tukihakikisha havutiwi na makundi mabaya, vilevile tunataka kuona kweli amejirekebisha,” alisema Nzowa na kuongeza:

“Ray C mwenyewe haoni lakini kila anapotoka, askari wanamuweka katikati. Kwa kifupi kipindi hiki, tumemuweka katikati yetu, kwani hata anapokuwa nyumbani, tunachunguza nani anaingia na amepeleka nini.”

Nzowa aliongeza kuwa kitengo chake kimeamua kumuweka kati Ray C kwa sababu mbili, moja ikiwa kubaini na kuwanasa wauzaji wanaomharibu mwanamuziki huyo, pili ni kufuatilia kama msaada uliotolewa na Rais Jakaya Kikwete umefanya kazi yake ipasavyo.

“Mheshimiwa (JK) alitoa msaada wa matibabu kwa Ray C kwa nia njema, vilevile dada huyo aliapa mbele yake kama hatarudia tena. Sasa ni lazima kufuatilia na kudhibiti asije kuingia kwenye vishawishi, akakiuka kiapo na matokeo yake alichokifanya mheshimiwa kikaonekana hakina maana,” alisema Nzowa.

Kwa upande mwingine, Nzowa alisema, hali ya Ray C inaendelea kuimarika na akaongeza: “Akili yake imetulia, anaweza hata kutunga nyimbo tofauti na alivyokuwa. Watu ambao anafungamana nao kwa sasa ni wazuri, siyo magenge ya wauzaji na watumia madawa ya kulevya.”

Ray C, alisharipotiwa kuwa na hali mbaya baada ya kutopea kwenye utumiaji wa madawa ya kulevya.

Hata hivyo, JK aliamua kujitolea kunusuru hali ya mwanamuziki huyo kwa kugharamia matibabu yake mpaka apone.

Takriban miezi mitatu uliyopita, Ray C alitinga Ikulu na kumshukuru JK kwa msaada aliompa, vilevile akawaambia Watanzania kwamba sasa anajisikia amepona na anaweza kufanya kazi.

 

 
Wednesday, 06 March 2013 06:23 Al News - Music
Print PDF

Q. Chillah Ma-DJ wamerogwa, wanapiga ngoma mbaya redioni

Galacha wa Bongo Fleva, Aboubakar Shaban Katwila ‘Q. Chilla’, amehamisha topiki ya uchawi kutoka kufanyiziwa na wasanii wenzake, sasa anawalilia Ma-DJ na watangazaji wa redio na televisheni kwamba nao wamerogwa.

Chillah alimweleza ripota wetu wiki iliyopita kwamba wanamuziki wengi kwa sasa ni wachawi, wanasafiri kwa nyota za wenzao kiasi ambacho wamefanya game la Bongo Fleva litawaliwe na ushirikina.

“Watu wamekuwa wachawi sana, wanaturoga sana nyota zetu sififie, hawa wanamuziki wachanga wanaoturoga sisi wakongwe, wamefikia hatua mbaya kwani wanawaroga mpaka Ma-DJ na watangazaji wa redio na televisheni.

“Ndiyo maana unaona siku hizi Ma-DJ na watangazaji wanacheza nyimbo mbaya kwenye redio na televisheni. Kuna ngoma kali sana hazisikiki kwa sababu zinabanwa na nyimbo mbaya ambazo zinapewa kipaumbele.

“Unaweza kudhani ni rushwa kama amabavyo wengi wanasema, siyo kweli kabisa. Ule ni uchawi kwa sababu Ma-DJ na watangazaji wengi wamerogwa kiasi ambacho wametoka kwenye mstari ulionyooka. Inabidi tukatae ushirikina kwenye game, la sivyo utatumaliza.”

Hivi karibuni, Chillah alishusha tuhuma nzito kwamba mwanamuziki Nasibu Abdul Juma ‘Diamond’ anasafiria nyota yake kwa sababu amemroga.

Diamond alijibu kuwa Chillah anamuonea wivu kwa mafanikio yake ndiyo maana badala ya kufanya kazi, anakaa kulalamika amerogwa jambo ambalo siyo la kweli.

 
Tuesday, 02 April 2013 20:47 Al News - Music
Print PDF

J Lo atia doa mchezo wa Kriketi India

Diva Jennifer Lopez ‘J Lo’, ametia doa sherehe za uzinduzi wa Ligi Kuu ya Kriketi nchini India, zinazotarajiwa kufanyika leo (Jumanne).

Chama cha Kriketi India, kilimwalika J Lo kuwa mtumbuizaji katika sherehe hizo za ufunguzi wa ligi kuu lakini mwanamuziki huyo alitanguliza mahitaji makubwa hatua za mwishoni.

Habari zinasema kuwa wiki moja kabla ya uzinduzi, J Lo alitaka Chama cha Kreketi India, kimkodishie ndege binafsi kubwa, itakayoweza kubebe msafara wake mkubwa.

Kingine, J Lo alitaka idadi kubw ya vyumba vya hoteli kwa sababu msafara wake una watu wengi, akataka pia mpishi wake binafsi naye agharamiwe, kwani ndiye atakayekuwa anampikia chakula chake siku zote atakapokuwa India.

Kutokana na mahitaji hayo, Chama cha Kriketi India, kiliamua kuachana na J Lo na badala yake, kikasaini mkataba na rapa, Pitbull ambaye anatarajiwa kutumbuza kwenye sherehe hizo leo.

 
Thursday, 28 March 2013 08:21 Al News - Music
Print PDF

Prof. Jay ajikamilisha kiujasiriamali

Akiwa anakaribia kuzindua studio yake mpya na ya kisasa ya kurekodi muziki, galacha Joseph Haule ‘Profesa Jay’, ameamua kujikamilisha kiujasiriamali kwa kufungua saluni ya kiwango cha juu kwa wanaume.

Saluni hiyo, ipo kwenye hatua za mwisho kukamilika na very soon itachukua nafasi kwa brand ya Professor Jay Classic Barber Shop.

Jay mwenyewe ndiye amekisanua hiki, akafafanua: “Professor Jay Classic Barber Shop ipo Msasani. Tunafanya muziki sawa lakini ni vizuri kuwekeza huku na huko.

“Nataka niwahakikishie mashabiki wangu kwamba saluni hiyo sijachungulia, isipokuwa nimeamua kujiwekeza kibiashara katika Nyanja tofautitofauti.”

Kuhusu muziki wake, Jay alisema: “Nina silaha nyingi sana, najiwekea muda wa kuachia ngoma mpya na kuwaacha watu waisikilize. Kwa zaidi ya miaka 20 ambayo nimekuwa kwenye huu muziki sitakiwi kuwa mtu kukurupuka.”

 
Tuesday, 26 March 2013 03:44 Al News - Music
Print PDF

MCD atangaza kurudi Twanga Pepeta bure

Mpiga tumba wa Bendi ya Mashujaa Musica, Sudi Mohamed ‘MCD’ ametangaza kwamba Bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ ndiyo nyumbani kwake, hivyo atakapoamua, atarudi bure.

MCD, aliyepata umaarufu mkubwa akiwa Twanga, amesema kuwa yupo tayari kurudi kwenye bendi yake hiyo ya zamani hata bure bila kulipwa chochote.

Alisema kuwa siku yoyote anaweza kurejea Twanga kwani ni kiwanja chake cha nyumbani na hakugombana na uongozi hivyo ikitokea wakati wa kufanya hivyo, hatakuwa na hiyana.

“Twanga ni kama nyumbani pia ni bendi iliyonilea na kunifunza vitu vingi kuhusu muziki hivyo sina tatizo nao naweza kurejea hata bila ada ya uhamisho,’’ alisema mpiga tumba huyo.

 
Friday, 22 March 2013 06:29 Al News - Music
Print PDF

Kisa wimbo wa Diamond, Mama Wema nusura amchape vibao DJ

Mama wa Wema Sepetu, Mariam Sepetu juzikati alitoa kali ya mwaka baada ya kumvaa Dj na kutaka kumchapa vibao kisa kikiwa ni kupiga nyimbo za aliyekuwa ‘mkwe’ wake, Nasib Abdul ‘Diamond’.

Tukio hilo lilijiri hivi karibuni nyumbani kwa Mtangazaji wa Clouds TV na Redio, Zamaradi Mketema, Mbezi Beach jijini Dar kulikokuwa na ‘bethidei’ ya mwanaye aitwaye Russel.

Wakati watu wakiendelea kuburudika, Dj aliweka wimbo wa Diamond wa Nimpende Nani ambapo ghafla mama Wema alionekana kuhamaki pale wimbo huo ulipofikia ile sehemu inayosema: ‘Yasiwe kama ya Wema Sepetu, kila siku magazeti’.

Mara mama huyo akiwa amefura aliinuka na kwenda kwenye meza ya muziki na kuuzima kisha ‘kumuanzishia’ Dj huku akimchimba mkwara kuwa hataki kusikia nyimbo za Diamond popote pale anapokuwepo.

“Hivi wewe Dj toka nifike ni nyimbo za Diamond, hakuna nyimbo nyingine? Nakuomba sehemu yoyote utakayoniona mimi usiweke nyimbo hizo, sawa… na hivi sasa badili wimbo,” alisikika mama huyo akisema kwa hasira.

Kufuatia mkwara aliochimba mama huyo, Dj alikuwa mpole hivyo kuachana na nyimbo za Diamond na kupiga nyingine ili kuepusha shari.

 
Tuesday, 19 March 2013 07:15 Al News - Music
Print PDF

Waingereza wabeba bango la kumshusha Bieber

Kitendo cha kuchelewa kwa saa mbili kupanda jukwaani, kimewaudhi Waingereza na sasa kuna kampeni nzito ya kumbomoa mwanamuziki janki, raia wa Canada, Justin Bieber.

Usiku waJumatatu ya wiki iliyopita, ndani ya Ukumbi wa London’s O2 Arena, London, Uingereza, Bieber alipiga shoo lakini amewaudhi mashabiki kwa sababu alichelewa.

Gazeti moja la Uingereza liliandika kuwa Bieber alipanda jukwaani akiwa amechelewa kwa saa mbili kutoka muda ambao ulitangazwa.

Limeandika kuwa sababu kubwa ya kuchelewa ni kitendo cha Bieber kutumia muda mwingi chumbani badala kutoka kuwahi mzigoni.

Gazeti hilo, liliandika kwamba Bieber alipogongewa mlango kwa ajili ya kuwahi shoo, alijibu: “Mashabiki ni wangu na nitatoka muda nitakaotaka.”

Hata hivyo, kauli hiyo imedaiwa kuwa imejaa uchochezi na kwamba hayo maneno hayakutamkwa na Bieber, isipokuwa ni chumvi ili kumchonganisha janki huyo na mashabiki wake wa Uingereza.

Madai zaidi kuhusu Bieber ni kuwa alishindwa kumtendea haki mtoto mwenye umri wa miaka 15 ambaye alishinda zawadi kukutana naye kwa ukaribu.

Imebainishwa kwamba Bieber alitumia muda ambao ni pungufu ya sekunde 10 kuwa karibu na mtoto huyo, hali ambayo imesababisha shindano lenyewe lionekane feki, kwani mshindi hakupata zawadi aliyostahili.

Vilevile, Bieber amepigwa zengwe kwamba alipokuwa anaingia kwenye klabu hiyo, alijifanya yupo ‘bize’ bila kuwajali mashabiki wake.

Kwa upande mwingine, kuna ambao wanasema kuwa kilichowachukiza Waingereza mpaka kuamua kumbomoa Bieber, ni kitendo cha janki huyo kutoka hotelini hadi ukumbini kwa msafara unaoongozwa na pikipiki zilizokuwa zinapeperusha Bendera ya Taifa la Canada.

CHANZO KIKAUA

Chanzo kilichodaiwa kipo karibu sana na Bieber, kilisema kuwa janki huyo alijifungia chumbani, akatumia muda mwingi kucheza game kwenye kompyuta badala ya kuwahi shoo iliyompeleka London.

Kilidai kuwa taarifa kwamba kulitokea hitilafu za kiufundi si ukweli, kwani Bieber, 19, alisababisha yote yatokee.

“Kuna mashabiki walikuwa na hamu sana ya kumuona, aliwafanya wamchukie. Kuna mama aliingia na wanaye, wamevaa fulana zenye picha na jina la Bieber, aliwaudhi sana,” kilisema chanzo.

MHARIRI AMCHANA

Mhariri wa habari za burudani wa Gazetu la The Sun, Gordon Smart, alisema: “Kuna staa wa muziki wa Rock aliniambia kuwa mwanamuziki anaweza kuchelewa jukwaani kama tu atakuwa hawaheshimu mashabiki wake. Bieber alifanya makosa makubwa na hastahili msamaha kwa aliyoyafanya.”

 
Monday, 18 March 2013 15:02 Al News - Music
Print PDF

Ngoma ya Jide na Profesa Jay yatikisa

Singo mpya inayokwenda kwa jina la Joto Hasira ya mdada mkongwe wa muziki wa Bongo Fleva, Judith Wambura ‘Lady Jaydee’ akimshirikisha galacha wa Hip Hop, Joseph Haule ‘Profesa Jay, imeshapenya na kukaa on top, kwani sasa inatikisa ile mbaya.

Melody na ujumbe ulioshiba, sauti tamu ya Jide, kiwango kikubwa cha kurap, swaga, styles ambavyo Jay amevionesha, kwa pamoja vimeibeba ngoma hiyo kiasi kwamba hivi sasa inabamba ile mbaya kwenye stesheni kibao za redio.


Hata video ya ngoma hiyo, pamoja na ukweli kwamba haina muda mrefu kihivyo lakini nayo inafunika, huku ikipokea chaguo la mara kwa mara kutoka watazamaji wa runinga.

Ngoma hiyo, inaelezea watu fulani ambao huhitaji kupewa sapoti kwenye mambo yao lakini baada ya mafanikio hujichimbia na kula peke yao.

“Tunalima wote, tunapanda wote, tunapalilia wote lakini mbona kuvuna hatuvuni wote?” ni sehemu ya mashairi yanayosika ndani ya wimbo huo.

Msisitizo wa ngoma hiyo, wote Jide na Jay wanasema kwamba sasa hawaangalii nyuma, kwani wanatengeneza fedha na kuzipa kwa heri shida, “we make more maney, rest in peace shida.”

 
Wednesday, 06 March 2013 06:28 Al News - Music
Print PDF

Justin Bieber alivyowehuka England

Dogo tajiri, Justin Bieber ambaye Ijumaa iliyopita alitimiza umri wa miaka 19, aliwehuka kimtindo ndani ya ardhi ya David Cameron.

Wiki iliyopita, Bieber akiwa ndani ya Jiji la Birmingham, alifanya matukio mawili ambayo yaliwafanya walioshuhudia wajiulize maswali bila kupata majibu.

TUKIO LA KWANZA; Jioni akiwa na wakufunzi wake, Bieber alikatiza mitaa kadhaa akiwa kifua wazi, akionesha mwili wake ambao umeshakubali mazoezi.

Janki huyo, mbali na kuacha kifua wazi, vilevile aliavaa suruali nzito ya kutepeta na kutokelezea ile ki-MC Hammer staili, hapohapo akaacha wazi nguo yake ya ndani.

Wakati anakatiza barabarani, Bieber alikuwa anaonesha kujiamini, huku akizionesha tatuu pamoja na miraba iliyojichora kutokana na mazoezi (six-pack).

Siku hiyo, Bieber akiwa na wapambe wake, waliendelea kukata mitaa ya Birmingham mpaka saa 9 usiku kabla ya kutia timu ndani ya British Luxury Club ambako walitafuna bata mpaka saa 11 alfajiri kwa saa za UK.

TUKIO LA PILI; Baada ya kutoka klabu, Bieber alionekana akiwa katika sura tofauti, sasa akiwa ni mwenye aibu, akikwepa asionekane.

Katika baadhi ya maeneo, alijaribu mpaka kuficha sura akitumia nguo aliyovaa, huku kapelo yake ya mchezo wa baseball ikimsaidia.

Imeripotiwa kwamba alikwenda kwenye mgahawa mmoja, akapata chakula cha Kilebanoni kabla ya saa 12:30 asubuhi hajarejea hotelini kupumzika.

 
Tuesday, 05 March 2013 06:26 Al News - Music
Print PDF

Thomas Ulimwengu ajiandaa kutoka na singo kali

Mshambuliaji wa Taifa Stars ambaye pia anaichezea Klabu ya TP Mazembe ya DR Congo, Thomas Ulimwengu, amesema nje ya soka Mungu kambariki sauti ya kuimba na kuongeza kwamba sasa anajiandaa kutoka na singo kali.

Ulimwengu alisema tayari ameshatunga nyimbo zake kadhaa ambazo zinaweza kukamilisha albam.

Alisema muda mwingi akiwa anapumzika baada ya kumaliza shughuli zake za soka, ndiyo huutumia kwa ajili ya kutunga nyimbo ili kujiweka ‘bize’.

“Mimi ni kijana mdogo na bado nina malengo mengi ili kukamilisha ndoto zangu, inabidi niweze kutumia kipaji changu kukamilisha ndoto hizo nilizonazo,” alisema Ulimwengu.

Ulimwengu ni Mtazania lakini anakichezea kikosi cha TP Mazembe cha DR Congo.

 

 

Page 1 of 12

<< Start < Prev 1 2 3 4 5 6 7 8 9 10 Next > End >>