Music | Lifestyle+Fashion | Antivirus | Love+Relationships | Business+Politics | Sport | TUMA Registrations

You are here:   HomeLove+Relationships
| + -

Love+Relationships

Friday, 03 May 2013 07:49 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Aunt Ezekiel, mumewe wakutana Sauzi

Mwigizaji Aunt Ezekiel ameonekana Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, akikwea pipa kumfuata mumewe, Dimonte Almousa, pande za Afrika Kusini.

Ripota wetu alimshuhudia staa huyo akikwea pipa mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya mumewe aishiye Dubai kumpa taarifa kwamba atakuwa Afrika Kusini kikazi hivyo wakutane kwa muda.

“Nakwenda Sauzi kwa muda wa wiki moja kwa ajili ya kukutana na mume wangu, sitakaa sana nitarudi Bongo kisha nitajiandaa kumfuata nyumbani kwetu Dubai,” alisema Aunt.

Hivi karibuni Aunt aliweka bayana kuwa hata iweje, kamwe hawezi kutengana na mumewe huyo.

 
Wednesday, 24 April 2013 19:07 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Mrembo adai kuambukiza Ukimwi wanaume 1500

Simulizi yake ni hii;

Nilizaliwa mkoa wa Dodoma na nilishi vizuri tu tangu utotoni na hata sikujihusisha na ngono hadi nilipomaliza form 4 mwaka 2006 baada ya kumaliza nilikuja hapa Dar kuishi kwa mama mdogo aliyeolewa hapa Mwenge.

Nilipata marafiki wengi tu na kuna kijana mmoja alinitongoza kwa muda mrefu sana na siunajua vijana wengi hutumia muda mrefu kutongoza ili msichana unadhani kwamba labda huyo anakupenda kumbe anataka tu ngono na wadada wengi sana hudhani kufuatiliwa kwa muda mrefu na mvulana basi huyo yuko serious kumbe hakuna lolote.

Nilimkubalia tukawa wapenzi ila nilikataa kuhusu kufanya mapenzi maana anayekupenda kiukweli sio uongo lazima asitake ngono kabla ya ndoa.

Kwa miezi kama 5 hadi 6 aliniambia kuhusu kufanya mapenzi nilikataa alitumia mbinu nyingi sana kwa kunibembeleza na hata kulia mbele yangu ili tufanye tu mara moja ila nilikataa, alisema atavumilia hadi siku ya ndoa yetu ambapo tulipanga kuoana mwaka sept 2009.

Siku moja aliniambia twende kwenye kumbi za starehe na mimi kwa sababu ya upagani na kumwamini pia kwa sababu nampenda nilikubali tulienda huko na kulikua na bendi fulani maarufu ya mziki wa dansi ilikua inatumbuiza.

Tulitafuta sehemu na kukaa na mpenzi wangu akaagiza pombe alianza kunywa huku akinionjesha, nilikataa kwa sababu nilikua sijawahi kunywa pombe katika maisha yangu yote, hata sijui alinishawishi vipi nilijikuta nakunywa kidogo kidogo na kwa kuwa tulikaa pale kwa muda zaidi ya masaa 5 nadhani nikunywa kama bia 3 au 4 japokua nilikua nakunywa kidogo kidogo tu tena kwa kunywesha na mpenzi wangu maana nikama nikua nanyweshwa kila baada kama ya dakika 25 ndipo nakunywa mara moja na sikujuia kama nakunywa pombe ila niliihisi tu naonja ili kumlizisha mpenzi wangu.

Ilipofika saa 10 alfajiri nilihisi usingizi na pia nilijiona wa tofauti najua nililewa hata kama sikujua kama nimelewa maana nakumbuka tulitoka pale huku amenishika mkono huyo mpenzi wangu. Tulikodo tax na kuondoka na siku hiyo aliniambia twende kwake alikokua amepanga chumba maana tulikua na usingizi sana nilikubali huku nikidhani hatuwezi kufanya mapenzi.

Tulifika salama na kuingia ndani ukweli pombe ni kichocheo cha ngono na ningekua mimi ndio Raisi wa Tanzania ningefunga bar zote. Nilijikuta natamani kufanya mapenzi na huyu mpenzi wangu hata alikua hana nia maana alijua atanichukiza sana na uhusiano ungekufa siku hiyo lakini kwa sababu ya pombe nilimwambia siku hiyo tufanye kidogo maana mwili wangu unataka.

Ni kweli siku hiyo kwa sababu ya pombe nilifanya mapenzi na huyo mpenzi wangu na baadae akanipeleka nyumbani baada ya wiki mbili maana tulikaa wiki mbili bila kuonana alikuja na kunieleza habari ambayo sikuihitaji katika maisha yangu maana nilikua nasikia tu kwa watu wengine lakini sio kwangu alisema ”JANE ISHI KWA MATUMAINI KUANZIA SASA”

Nilidhani utani lakini aliniambia kuwa yeye ana UKIMWI tangu miaka mitano iliyopita na anapenda tu ngono maana hawezi kuacha.

Nililia sana na baada ya wiki moja baadae nikaenda kupima na kukutwa nina ugojwa ambao niliusikia tu kwa watu na chanzo cha yote ni pombe, kupenda starehe,disko na upagani unaotusumbua wanadamu wengi.

Nilikua na UKIMWI na kwa hasira maana mpenzi wangu alihamia Arusha huku akisema neno moja la mwisho kwamba ”shetani amemtuma kuwaambukiza wanadamu UKIMWI”

Sikujua, sikujua, sikujua, sikujuaaaaaaaaa, basi tu ooh YESU nihurumie mimi leo.Nilibebeshwa mzigo ambao haukunistahili mimi. Hata leo hua najiuliza kwamba nilijitunza kwa miaka 23 yote lakini pombe na huyu wakala wa shetani wamenifanyia hivi. Baada ya kujua nina UKIMWI na hali hiyo nikaikubali na kulikua na kundi kubwa sana la wanaume ambao walikua wamewahi kunitongoja na niliwakataa sana kwa sababu hii niliwakubali ili nami nife na wengi.

Nilianza kumkubali kila mmoja na kuna baba mmoja ambaye ana wake 3 niliwahi kumtukana sana kipindi cha nyuma kila aliponitongoza lakini wakati huu nilimkubali na hakuamini na tukafanya ngono tena bila kinga na akaniaachia pesa laki 6 kama zawadi ya kumkubali kumbe naye hakujua kuwa namwambukiza na hata leo hua nawahurumia tu wale wake zake ambao wana UKIMWI uliotoka kwangu.

Kiukweli tangu may 2009 hadi 2012 nimeshatembea na wanaume zaidi 1500 maana ilifika kipindi nala na wanaume 3 kwa siku na lengo langu niwakomeshe kama mimi nilivyokomeshwa na nina uhakika kutokana na mimi wameambukizwa UKIMWI wanadamu zaidi ya 10,000 na hili tangazo la ”TUKO WANGAPI” huwa linaniliza kila siku maana hata mimi najua kabisa nilianzisha mtandao kama huo wa ngono kwa idadi kubwa sana ya watu.

Nimeokoka miezi 7 iliyopita na siku naombewa nilikutwa na mapepo mengi sana na hata waombeaji wakashangaa. Ningejua ningeokoka tangu nikiwa na miaka 5 lakini ndio hivyo sina jinsi wala uwezo wa kubadirisha hali hiyo.

Na naomba kila atakayesoma ujumbe huu ajue kuanzia leo kuwa pombe ni dhambi pia kwenda disko ni dhambi,kuuza pombe ni dhambi na kila kichochoe chochote cha dhambi ni dhambi. Hadi sasa mtu yeyote hawezi kujua kama nina UKIMWI na sijui MUNGU ana mpango gani na mimi maana kwake yote yanawezekana. Nauamini uponyaji wake na sijawahi kutumia ARV hata siku moja na afya yangu iko sawa tu na huwezi hata wewe kujua kama uovu huu nimefanya mimi.

Ndugu zangu kama una UKIMWI nenda kanisani ukaombewe na kama una akili mpe YESU maisha yako maana pia baada ya kifo ni hukumu. Yasalimishe maisha yako kwa YESU na usiambukize wengine tena.

Mimi tangu niokoke sijawahi kufanya mapenzi tena na sitafanya hivyo wala sitaolewa na mtu yeyote maana yatosha kwa uovu niliofanya na hadi sasa wapo ninaowajua zaidi ya 15 wameshafariki na nilihudhulia misibani huku nikijua kabisa chanzo ni mimi.

Mwisho nawashauli wababa kulidhika na wake zao na wamama pia lidhikeni na waume zenu, vijana ambao hamjaoa wala kuolewa subiri hadi utakapooa au kuolewa na kabla ya kuolewa au kuoa kapimeni kwanza kwani wenye UKIMWI ni wengi kuliko unavyozani.

Fuata unachofundishwa kanisani na pia soma BIBLIA na uwe mtakatifu.

MUNGU akubariki

Ni mimi Jane,
Mwenge, Dar es salaam
Tanzania

 
Tuesday, 23 April 2013 14:53 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Kaka amfundisha dada yake ‘kitchen party’ kitandani

Katika siku za mwanzo tu uhusiano wao, Martha alimpa utambulisho boyfriend wake Jacob: “Sweetheart, huyu ni rafiki yangu anaitwa Roy, ni mshkaji wangu wa karibu, mimi na yeye ni kama kaka na dada, siri yangu yake, yake yangu. Baadaye ukiniona naye usije kunionea wivu.”

Jacob aliitikia kisha maisha yakaendelea. Penzi likakua, Jacob alimvalisha Martha pete ya uchumba baada ya utambulisho kwa wazazi kufanyika na kukubalika. Taratibu za ndoa zikashika kasi lakini kuelekea kuoana, kuna jambo la kushangaza likajionesha.

Siku moja asubuhi, Jacob alifika nyumbani kwa Martha kwa ajili ya kumpelekea matumizi. Alikukuta mlango wa sebuleni upo wazi, akaingia na kupitiliza kabisa chumbani. Akastaajabu kumkuta Roy amelala, amejiachia kitandani.

Jacob akasalimia: “Kaka mambo vipi?”

Roy akajibu: “Safi kabisa bro.” Namna Roy alivyojibu, alionesha kujiamini kupita kiasi. Mara, Martha naye akatokea choo cha chumbani akiwa amejifunga kanga moja tu!

“Waooo baby umenisapraiz leo asubuhiasubuhi,” Martha alisema.

Jacob akamtoa Martha sebuleni ili wazungumze. Ile wanaketi tu, Martha akalianzisha: “Baby usishangae kumkuta Roy hapa, aligombana na mkewe, kwa hiyo ikabidi aje alale hapa.”

“Kwa nini aje alale hapa tena kitandani kwako kabisa?” Jacob aliuliza.

“Ndiyo sweetheart, si unajua Roy anavyonipenda na kunizoea mimi dada yake? Ikabidi aje alale hapa, vinginevyo labda angekwenda kulala hotelini, sasa gharama za nini?” Martha alijibu kwa mtindo wa kuhoji.

“Ukaingia chooni kuoga, ukatoka na kanga moja mbele ya Roy, eti kaka yako. Unawezaje kunishawishi nikuamini kuwa wewe na yeye siyo wapenzi?” Jacob aliuliza.

Martha alijitetea, Jacob akamwambia amemwelewa. Alimkabidhi fedha za matumizi kisha akaaga kuondoka. Martha alimsindikiza, akahakikisha Jacob anaingia kwenye gari na kuanza kuondoka ndipo naye akaingia ndani.

Jacob hakufika mbali, alipoangalia kwenye vioo (side mirrors) na kumuona Martha anarudi ndani, aligeuza gari. Alipofika alipaki na kuanza kutembea kwa kunyata. Mlango wa sebuleni alikuta upo wazi, akapitiliza mpaka mlango wa chumbani.

Pale kwenye mlango wa chumbani, akasikia sauti ya Roy ikiuliza: “Vipi jamaa yako ameondoka?”

Martha akajibu: “Bwege yule ameshaondoka, ila kaniuliza maswali magumu? Inaonekana ameshaanza kutushtukia.”

Jacob aliposukuma mlango, aliwakuta Martha na Roy wamelaliana. Walipomwona walishtuka sana, mwenyewe akawaambia: “Endeleeni starehe zenu, mimi bwege nilikuwa napita tu!” Baada ya hapo akaondoka zake.

Kuanzia siku hiyo, Jacob alipokea SMS mfululizo kutoka kwa Martha na Roy wakimwomba msamaha kwa waliyomtendea lakini hakujibu hata moja. Walipiga simu lakini hakupokea. Upande wa pili, Martha alimtupia lawama Roy: “Ona umeniharibia ndoa, nitafanya nini mimi na wewe una mke wako?”

Baada ya wiki tatu, Jacob aliwaita Roy na Martha nyumbani kwake ili waende wakazungumze na kuyamaliza. Walienda haraka sana. Walipofika sebuleni, Jacob aliwaambia waende mpaka chumbani. Haikuwa shida, Martha anakijua chumba, kwa hiyo wakaingia.

Mbona ilikuwa sinema? Jacob alikuwa amelala akiwa amemkumbatia mwanamke mrembo anayeitwa Rosemina. Huyo Rosemina ni mke wa Roy. Palepale Roy na Martha waliteleza na kujikuta wamekaa chini kwa mshtuko. Picha ilikuwa wazi kuwa Jacob na Rosemina ni wapenzi, maana hata pale kitandani hawakuwa na nguo iliyowasitiri.

Jacob akafunguka: “Nyie si mlisema mimi ni bwege, sasa nimeamua kuwaonesha ubwege wangu, kuanzia sasa ninyi nendeni mkaone, mimi nitamuoa Rosemina wangu hapa. Nimempata kwa urahisi kwa sababu naye alikuwa ameshachoshwa na tibia zenu, mnajifanya kaka na dada kumbe mahasidi wakubwa. Na mimi huyu ni dada yangu na hapa namfundisha ‘kitchen party’ ya kitandani.”

 
Thursday, 18 April 2013 06:29 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Jokate amcheka Uwoya kupitiwa Diamond

Mwanamitindo Jokate Mwegelo ‘Kidoti’, ameangua kicheko baada ya kusikia mwigizaji Irene Uwoya kunaswa hotelini na Nasibu Abdul ‘Diamond’.

Jokate aliangua kicheko hicho juzikati jijini, Dar wakati alipozungumza na ripota wetu na alipogusiwa kuhusu suala la Uwoya kunaswa na Diamond, alicheka sana huku akimshangaa.

“Hahaha sasa ndiyo nini tena, yeye si aliwahi kunisema mimi nakwapua mabwana? Sasa leo imetokea kwake tena!” alisema Jokate.

Aliongeza: “Kumbe yale yalikuwa maneno maneno, mwisho nay eye ametoka na Diamond, kwa kweli inachekesha sana. Naona kama sinema vile.”

Machi 25, mwaka huu, Diamond na Uwoya, walinaswa kwenye hoteli moja yenye hadhi ya nyota tano, iliyopo Mbezi Beach, Dar es Salaam.

Ilielezwa kuwa Diamond na Uwoya, walilala kwenye hoteli hiyo, chumba namba 208, wakiingia saa 8:24 usiku kisha wakatoka kati ya saa 9:00 na saa 9:13 mchana.

 
Thursday, 11 April 2013 10:57 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Mama alipompa mwanaye huduma ya faragha usiku mzima

Mama Moses ni mwanamke wa kimjinimjini, alianza kuwajua wanaume mapema sana. Akiwa na umri wa miaka 16, alipewa ujauzito na jamaa aliyekuwa kondakta wa daladala kwa wakati huo. Hakuwa na jinsi alijifungua mtoto wa kiume, akamwita Moses.

Kwa sasa Mama Moses ana umri wa miaka 44, Moses ana miaka 28. Mtu na mwanaye wanaishi kama wazungu. Maisha yao si haba, kwani miaka 19 iliyopita, Mama Moses alimliza mzungu mmoja kiasi kikubwa cha fedha, baada ya hapo akawekeza kwenye biashara mbalimbali, ikiwemo maduka Kariakoo na akawa anafuata mizigo China.

Moses ni mtoto wa pekee, kwa hiyo maisha yake yakawa kutumbua fedha za mama yake. Alizitumia kuendesha magari makali akiwa na umri mdogo kabisa. Alihakikisha anatoa ule mkong’oto wa baba na mama kwa warembo tofautitofauti, ikiwemo wanafunzi.

Hakuishia hapo, Moses alibeba mpaka mizigo inayomzidi kimo. Alitoka kimapenzi na wanawake wenye umri kumzidi hata mama yake. “Ninapopata jimama la ukweli, lililonizidi umri nainjoi sana. Hawa watoto nimewazoea, hawanipi stimu kabisa,” Moses aliwahi kumwambia rafiki yake Slay.

Kwa upande mwingine, Mama Moses tangu afikishe umri wa miaka 40, hakutaka kabisa kushiriki mapenzi na wanaume wenye umri mkubwa zaidi yake. “Zamani nilikuwa natembea na mibaba ili nipate fedha, sasa hivi hela ninayo, nataka vijana tu wanipe raha,” hiyo ni kauli ya Mama Moses, akimwambia shosti wake Monica.

“Hivi wewe Moses huwezi kuangalia warembo wa saizi yako? Tabia gani ya kutembea na mimama mikubwa, tena mingine inaweza hata kunizaa,” Mama Moses aliwahi kumwonya mwanaye.

“Mama wewe ndiye unanikata stimu, unatoka na vijana wadogo saizi yangu, wengine hata mimi nawazidi umri,” Moses alimjibu mama yake. Pamoja na hivyo, hakuna kati yao aliyekoma.

Kuna siku moto uliwaka nyumbani kwao. Mama mtu alianza kumtuhumu mwanaye kuwa ametembea na rafiki yake Monica. “Wewe Monica si ni mama yako kabisa? yule ni rafiki yangu wa siku nyingi, wewe unajua lakini umetembea naye bila woga,” Mama Moses alimuwakia Moses ambaye naye alijibu: “Kweli mama mkuki kwa nguruwe, wewe ulifurahi sana ulipotoka na mshakaji wangu Aslay.”

Maisha yalizidi kwenda kasi, siku moja Moses akiwa klabu na marafiki zake, mara Jaca ambaye ni mshakaji wake mwingine aliingia. Walipiga stori mbalimbali lakini katikati ya mazungumzo, mmoja wa marafiki wa Moses alimuuliza Jaca ni kwa nini alichelewa klabu?

Jaca akajibu: “Leo jionijioni nilikutana na bonge la jimama, likanizimia halafu lina mawe kinoma, nikaona siyo vibaya ngoja nijiweke. Tulikula bata, tukaziua bia kama tumerogwa vile, baada ya hapo tukazama zetu chumbani kwenye hoteli moja hapo kati.

“Kabla ya kuanza mambo, machale yakanicheza. Ikabidi nimsimamie yule jimama aendelee kunywa, alewe ili nimtoroke. Alipolewa nikamkimbia zangu ndiyo maana mnaona nimechelewa. Maradhi mengi jamani, ukimwi upo.”

“Acha uzembe wewe, kwani hakuna kondomu?” Moses alimjibu Jaca. Papo hapo akaomba aelekezwe hoteli na chumba ambacho amemwacha huyo bi. mkubwa. Maelekezo yalifanyika, Moses ikabidi ajipe stimu kwa kupiga pombe za kutosha ndiyo amvae jimama aliyeogopwa na Jaca.

Baada ya kujitwika pombe za kutosha, Moses aliongozana na Jaca mpaka hotelini, wakapanda ghorofani mpaka kwenye chumba husika. Jaca aliingia kwanza kuhakikisha mazingira yapo salama, alipojiridhisha, alizima taa, halafu akatoka nje.

“Sasa wewe ukiingia ndani, anza kazi. Mama yupo hoi, usiwashe taa atakushtukia mapema,” Jaca alimpa maelezo Moses ambaye aliyapokea kisha akaingia ndani. Alipofika tu, alisoma gizani na kujua mahali kitanda kilipo na bi. mkubwa akiwa amejaa tele.

Akavua nguo harakaharaka, kisha akahamia kwa yule bi. mkubwa, akamchojoa kiwalo kimoja baada ya kingine. Alipofikia usawa wa kufuli, jimama lilijigeuza kama mzigo kisha akazungumza kwa sauti ya pombe: “Safi baby, unataka kunipa raha.”

Moses wala hakujibu, alichokifanya kwa wakati huo ni kumwandaa bi. mkubwa, tayari kwa shughuli inayofaa eneo walilopo. Jimama akawa anahangaika huku na huko, pombe zikawa zinamezwa na ule mchezo aliokuwa anafanyiwa. Mwisho mechi ikaanza.

Ilikuwa mechi yenye kila aina ya kashkashi za utamu kwa pande zote mbili. Moses alijitahidi kucheza salama, kila baada ya mchakamchaka mfupi, alichomoa daruga kuhakikisha kama kiatu kipo, kimevuka au kimepasuka. Aliporidhika kipo aliendelea kwa ari, nguvu na kasi zaidi.

Baada ya mchuano, wote walipitiwa na usingizi. Palipokucha, mwanga ukiwa umeshaingia chumbani, yaani siyo giza tena, Moses ndiye alikuwa wa kwanza kuamka. Akakumbuka matukio ya usiku uliopita, pombe zilishamwisha, akamwangalia jimama aliyepata naye raha usiku mzima.

“My God,” Moses alijikuta akitamka maneno hayo kwa mshangao. Ni maneno hayohayo ndiyo yaliyomwamsha yule bi. mkubwa ambaye mpaka wakati huo, alikuwa hana nguo hata moja.

Macho yakawatoka wote wawili, hakuna aliyethubutu kufungua kinywa kuzungumza chochote, kwani yule bi. mkubwa hakuwa mwingine, bali ni Mama Moses, kwa hiyo mama na mwana walipeana huduma ya faragha usiku mzima bila kujuana.

 
Tuesday, 02 April 2013 21:26 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Mimba yamkubali Kim Kardashian

Muonekano wa mtangazaji mwenye jina kubwa duniani, Kim Kardashian, unathibitisha kwamba ‘kibendi’ kimemkubali mdada huyo.

Kim ambaye ujauzito alionao ni matunda ya uhusiano wake wa kimapenzi na rapa, Kanye West, amechambuliwa kuwa hivi sasa amependeza zaidi, kuliko mwanzo.

Pamoja na kupendeza, imedaiwa kuwa Kim amekuwa mmama zaidi, hivyo kupoteza ile ‘shepu’ yake ya kiuanamitindo.

Hata hivyo, Kim mwenyewe anatetea muonekano wake kwa kusema: “Nipo kwenye mapenzi makubwa sana hivi sasa. Najikubali nilivyo, nina furaha sana.”

Akaongeza: “Ni kweli katika maisha yangu, napenda kupungua mwili na uzito ila sasa hivi nanenepa. Sina jinsi, nakubali hivyo kwa sababu mabadiliko yangu yanatokana ujio wa mtoto wangu.”

Kuhusu nini asichopenda kwa mtoto wake, Kim alisema: “Sihitaji mwanangu aje kwenye ulimwengu wa kusumbuana na maisha haya ya umaarufu, sitaki kabisa aje huku.”

 
Tuesday, 02 April 2013 20:52 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Jourdan: Bieber ananitongoza, simtaki

Mwanamitindo Jourdan Dunn, amesema kuwa baada ya mwanamuziki janki lakini tajiri, Justin Bieber, kuachana na patna wake, Selena Gomez, alianza kumgeuzia kibao yeye.

“Alianza kunitongoza lakini nimemkatalia,” alisema Jourdan, alipoliambia gazeti moja maarufu la England.

Jourdan akaongeza: “Ananiambia mimi ni mzuri sana. Wakati mwingine ananiambia nina matiti mazuri.”

Mwanamitindo huyo anaponda: “Sijavutiwa na Bieber, sijaona kitu cha kunifanya niwe naye. Nimekuwa nikimkatalia, namwambia hawezi kuwa na mimi.”

 
Wednesday, 27 March 2013 07:03 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Si umeona raha kuonja utamu wa shemeji yako?

“Judi, huyu ndiye shemeji yako Malcolm. Wenyewe tunasubiri kufunga zetu ndoa,” Jessica alimtambulisha Judith kwa mchumba wake, kisha akaendelea: “Nikimaliza tu chuo, mwenzako tunaoana.”

Haikupita wiki tatu, Malcolm akamlalamikia Jessica: “Yule rafiki yako mshamba sana, ananitumia SMS za ajabuajabu, sijui ananitaka nini.” Jessica alihamaki sana, kisha akataka kuona hizo SMS. Kweli baada ya kuziona, aliridhika kwamba Judith anamtongoza Malcolm.

Kilichomdatisha Judith mpaka akawa anahaha kumsaliti rafiki yake siyo kingine, bali ni maisha. Malcolm ni mfanyabiashara ambaye mpaka wakati huo alishapiga hatua kubwa. Kutokana na hali hiyo, alijitahidi sana kuyaweka vizuri maisha ya Jessica.

Kitu gani akitake akose? Gari la kutembelea aina Toyota Opa, kila siku anawaacha vibaya wanafunzi wenzake kwa mavazi ya gharama na pafyum ghali. Judith akahisi kwamba anaweza kumteka Malcolm na kupata huduma zote muhimu.

“Yule Jessica hana lolote, wewe ni mzuri kuliko yule kinyago cha mpapure,” haya ni maneno yaliyomwongezea jeuri Judith kwamba anaweza kumpindua Jessica kwa Malcolm kwa sababu marafiki zake humwambia yeye ni mlimbwende zaidi.

“Yule kinachombeba ni vipodozi, kama ataachwa bila vipodozi mbona yule ni shombo tu. Nakuhakikisha hakuna mwanaume anayeweza kuwaona wewe na Jessica halafu akampenda Jessica, lazima akupende wewe,” Judith alivimbishwa kichwa na maneno hayo.

Judith, alitamani naye aanze kumiliki gari, atinge mavazi ya gharama kama ilivyo kwa Jessica. Aliamini mwanaume anayeweza kumfanya aishi maisha ya aina hiyo ni Malcolm. Akaona njia sahihi ni kufanya mapinduzi. Akaamua kumtongoza Malcolm.

Kitendo cha Malcolm naye kumwambia Jessica, kiliibua tifu lisilopimika. Malcolm hakuwaza kama Jessica angekasirika kwa kiwango hicho. Ilibidi atumie juhudi zote kumbembeleza lakini haikuwezekana, mwisho ilibidi wakubaliane jambo moja.

“Si anakutongoza? Mkubali halafu utumbee naye kabisa ili tumkomeshe,” Jessica alimwagiza Malcolm.

“Hapana Jessica, nitakuwa nimekukosea heshima, vilevile tutamuua mtoto wa watu,” Malcolm alisema.

“Mimi ndiyo nataka, hutanivunjia heshima, bali ndiyo utakuwa umeniheshimu. Ukikataa tunaachana,” Jessica alimtisha Malcolm ambaye aliamua kufanya kile ambacho kitamfurahisha mwenzi wake anayetaraji kufunga naye ndoa.

Kwani zilipita hata siku mbili? Malcolm na Judith walikuwa kitandani ndani ya Hoteli C3 iliyopo Masaki, Dar es Salaam. Mandhari ya chumba ilikuwa bambamu, shughuli ya utangulizi ilianza kabla ya mechi yenyewe. Ilikuwa kazi kwelikweli!

Judith alijituma siyo kawaida. Alifanya kila awezalo kuhakikisha anamfanya Malcolm amuone yeye ndiye bora kuliko Jessica. Umeshawahi kuona mtoto wa kike anakata nyonga katikati ya kuta nne? Umeshashuhudia mrembo anaachia kilio cha mahaba? Siku hiyo Judith alitia fora.

“Mpenzi wangu ni wewe tu, sina mwanaume mwingine,” Judith alimwambia Malcolm wakati mchezo umefika mwisho. Judith alikuwa na furaha lakini Malcolm alikuwa kama mtu mwenye wasiwasi, kuonesha kwamba hakufurahishwa na kilichotokea.

Kwa uchovu, Judith alitoka kitandani, akaketi chini kwa kunyoosha miguu, huku mgongo wake akiuegemeza kwenye kitanda. Ghafla mlango ukafunguliwa, Jessica akaingia chumbani akiwa anatabasamu. Judith nusura akimbie.

“Wala usikimbie, kuwa na amani kabisa,” Jessica alimwambia Judith kisha akaongeza: “Umeona raha kuonja utamu wa shemeji yako? Basi vizuri, sasa pokea na huo ukimwi ili wote tuishi kwa matumaini. Mimi na Malcolm ni waathirika, tuliikubali hali yetu, sasa tunaishi kwa matumaini.”

 

 
Tuesday, 26 March 2013 03:46 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Mapenzi bora hupitia katika mzani, jifunze kupima na ‘kubalansi’

Hivi karibuni, niliandika mada “mahaba niue ni matokeo ya kuokosea vipimo vya mapenzi.” Huo ndiyo ukweli na makala haya ni maarifa kwako ili upate namna bora ya kuujua mzani wa mapenzi, kupima na kujua kutengeneza ulinganifu (kubalansi).

Huko nyuma, nimewahi kuandika mada inayosema, “Mapenzi ni matamu lakini siyo rahisi”. Nilieleza kwa upana jinsi ya kukabili. Leo nimekuja na muongozo wa jinsi ya kufanya ili uyaweze mapenzi na kuushinda ugumu uliopo.

Mada hii siyo tu lengo lake ni kukufanya ujue mzani, kuyapima mapenzi na kubalansi, pia itakufanya uyaelewe mapenzi. Si kukimbilia kuacha pale kunapotokea tofauti za hapa na pale na mwenzi wako wa maisha. Uvumilivu unahitajika, amini kwamba utamu wote unaoyazunguka ‘malavidavi’ kuna ugumu mkubwa.

Hapa tunazungumzia elimu zaidi inayoweza kukukomboa wewe kwa kuheshimu hisia za mwenzako na wakati huo huo ukawa unajali za kwako. Kwa pamoja ndipo utaweza kufanikiwa kuwa na moyo tulivu katika nyakati zote.

Ukiheshimu hisia za mwenzi wako na ukawa unajali za kwako, itakusaidia kukufanya uwe na tumaini chanya wakati wote. Wakati wa matatizo, hasa kipindi ambacho hampo kwenye maelewano mazuri, utabaki na imani kwamba yote yatakwisha.

Penda kuamini kuwa “hili nalo litapita” kwamba wakati ambao mwenzi wako amenuna, hataki kuzungumza na wewe, unachopaswa kufanya ni kuheshimu hisia zake na uamini kwamba mwisho atatulia na uhusiano wenu utaendelea kwa maelewano makubwa.

Ukitaka kulazimisha awe mchangamfu kwako kipindi ambacho amenuna, ni sawa na kukaribisha matatizo zaidi. Ni vema kuelewana, watu wengi wanakosea katika uhusiano wao kwa sababu hawatumii busara ili kuwawaelewa wenzi wao pindi wanapoonesha hali tofauti.

Busara iendelee kuchukua nafasi. Maneno “hili nalo litapita” liwe somo kwako. Kwamba leo umerudi nyumbani, umetaka chakula cha faragha, mwenzako amekwambia hajisikii vizuri. Hutakiwi kupandisha mizuka na kusababisha nyumbani pasilalike kwa siku hiyo.

Badala yake unapaswa kuvumilia. Jiulize mmefanya tendo mara ngani katika uhusiano wenu, iweje siku hiyo akwambie hajisikii? Ukilazimisha ni sawa na kumfanyia mwenzako ubakaji. Si ajabu akikuona unakuwa mkali, akakubali kukupa kwa shingo upande lakini si kwa ridhaa yake.

Mapenzi ni matamu lakini siyo rahisi kwa maana, nyakati nyingine utalazimika kuvumilia mambo ambayo pengine yakakuumiza. Mko wawili na kujenga tafsiri ya mwili mmoja. Pengine hata makundi yenu ya damu ni tofauti. Ilivyo maumbile yenu ni hasi na chanya ndiyo na damu zenu zilivyo.

Tofauti hiyo mnaielewa na kuikubali, iweje siku ukirudi nyumbani unamkuta amenuna na hataki kuzungumza na wewe ushindwe kuelewa? Hapo ndipo uvumilivu wako unahitajika. Ni kipindi ambacho busara zako zinapaswa kufanya kazi kwa asilimia 100. Usilazimishe afanye upendavyo wakali mwili wake haupo tayari.

Unaingia faragha na mwenzi wako. Ameshindwa kukuridhisha kabisa. Ni hekima zako kutambua kwamba siku hazilingani. Mbona siku nyingine alikupa mambo mazuri mpaka ukasema ‘poo’? Tatizo ni nini? Pengine nishati za mwili wake kwa siku hiyo hazipo sawasawa na hata yeye mwenyewe hajui.

Ukimkejeli kuwa hajiwezi ni sawa na kumchinjia baharini. Siku zinazokuja atashindwa kabisa. Si kwa sababu uwezo wake ni mdogo, la hasha! Maneno yako ya kejeli na dharau ndiyo yatakayoufanya moyo wake usinyae na kukuogopa ndani kwa ndani. Fikra zake zitashambuliwa na ugonjwa hatari.

Si ugonjwa unaosababishwa na kirusi, hapana. Ni gonjwa la maneno litakaloshambulia ubongo wake. Kila mara kabla ya kuingia mchezo atakuwa na maswali ya kujiuliza. “Sijui leo nitashindwa tena?” “Nikishindwa itakuwaje?” “Atanitukana tena?” “Hivi mimi ni mgonjwa?”

Mwisho wa maswali hayo atahitimisha kauli kwa kusema: “Inawezekana mimi ni mgonjwa kweli ndiyo maana nashindwa kazi.” Amini kuwa kauli hiyo ndiyo ugonjwa hatari ambao utashambulia hisia zake na kuusababisha mwili ushindwe kufanya kazi sawasawa.

Ukitaka kuendelea kufurahia mapenzi ni vizuri umpe moyo mwenzi wako pale inapoonekana ameshindwa kutekeleza kazi ya faragha inavyotakiwa. Kaa naye vizuri na umueleze kwa lugha laini kwamba baadaye au siku inayofuata mtafanya tena kikamilifu na hakutakuwa na kushindwa.

Ikibidi msifie, mwambie kuwa yupo kamili kwa sababu kila siku mnapoingia kazini huwa unatosheka. Mueleze kuwa siku hiyo anasumbuliwa na uchovu au hajisikii vizuri. Maneno hayo utayaona madogo lakini yatamjenga ipasavyo. Yatamrejeshea ari na afya, kwa hiyo siku nyingine hatakuogopa.

Mapenzi ni matamu lakini siyo rahisi. Hii imesababisha watu wengi kushindwa kushirikiana vema na wenzi wao. Jambo dogo la kumuelewesha mwenzake linakuwa tatizo mpaka uhusiano unageuka shubiri. Wawili walioitana majina matamu na yenye kupendeza, wanageuka maadui.

Wanatangaziana sifa mbaya. “Yule muoneni hivyo hivyo kwa nje, hajiwezi kabisa kitandani.” Ni maneno ambayo si mageni. Yanasababishwa na watu kutotambua thamani ya mapenzi, ugumu uliopo ili iwe rahisi kwao kupata alama A kwenye uhusiano wao. Mapenzi ni magumu lakini ni rahisi sana.

Kanuni ni moja tu, kuwa mwelewa. Unaona mwenzi wako anashindwa kukufikisha unapopataka, wewe una jukumu la kumwelewesha. Mfahamishe maeneo ambayo anatakiwa ayafanyie kazi ili ufurahie tendo. Amini kuwa ukifanya hivyo, itakuwa rahisi kwako. Mapenzi ni matamu kama utayajua na kuyaweza.

Kuna maswali ya kujiuliza kuhusu mapenzi. Hayo ndiyo yatakuwezesha kutambua kama unatosha kuendelea na mwenzi wako au kinyume chake. Yatakusaidia kufurahia maisha yako ya kimapenzi.

Itaendelea wiki ijayo.

Mapenzi bora hupitia katika mzani, jifunze kupima na kubalansi - 2

Mapenzi ni matamu lakini siyo rahisi. Mada hiyo niliyoiandika kwenye gazeti hili kwenye matoleo yaliyopita ndiyo imeleta muendelezo huu. Hii ni sehemu ya pili na lengo lake ni kuushinda ugumu uliopo na kuyaweza mapenzi kwa asilimia 100.

Jambo la muhimu ni kwamba usije ukaingia kwenye uhusiano ukidhani kila kitu ni chepesi. Unatakiwa kujipanga, halafu uwe mdadisi kisha upite njia inayostahili.

Ugumu mkubwa ambao upo kwenye mapenzi ni pale mtu anapotaka aoneshwe upendo kulingana na jinsi anavyopenda. Inapotokea anabaini tofauti kati ya anavyopenda na anavyopendwa inakuwa shida kubwa. Hataki kupenda zaidi, eti ataonekana wa bei nafuu.

Kila mtu anataka apendwe zaidi. Kwa nini wewe usiwe wa kwanza kujitoa kumpenda mwenzi wako kuliko yeye anavyokupenda? Ni mtihani mdogo lakini unawashinda wengi na kusababisha mvutano.

Uzoefu unaonesha kuwa watu wengi hawana imani na wenzi wao. Dosari ndogo inaweza kuwafanya wajenge imani kuwa wenzi wao hawawapendi. Kila mmoja analalamika kivyake. “Hanipendi kama mimi ninavyompenda.” Ugumu wa mapenzi huanzia hapo.

Nimeshachambua mengi huko nyuma. Kwa nyongeza, leo nakutaka ujiulize maswali yafuatayo ili uepukane na ugonjwa wa moyo, badala yake, mapenzi kwako yawe kitu rahisi ambacho utakimudu kwa asilimia 100.

*Tazama unavyojisikia pale unapopenda. Je, unapopenda unajisikia vizuri hata kama umpendaye hakupi upendo kama ulionao kwake? Je, kumpenda mtu, ni lazima naye akupende kwa kiwango hicho hicho? Kama ndivyo, ni kwa nini?

*Unajisikia unapendwa hata kama mwenzi wako hayupo? Kama sivyo, ni kwa nini? Je, unajikubali na unaridhika kwa sifa ulizonazo?

*Unafanya vitu kwa ajili ya mpenzi wako? Hata kama hutaki kufanya, je unajitahidi kutekeleza ili kuliweka penzi lenu hai? Unafanya kwa ajili ya mapenzi yake na unahitaji kila unachofanya, naye akufanyie hivyo hivyo?

*Je, umewahi kumueleza mwenzi wako vitu ambavyo ukifanyiwa vinaweza kukufanya ujisikie kupendwa? Amewahi kutekeleza vitu hivyo kwa ajili yako? Kama bado, umewahi kuvumilia na kumfundisha taratibu?

MNAFANANA?

Swali hili lipe uzito. Inawezekana kwenye maswali ya juu ukawa umevuka vizuri. Pamoja na hivyo, haioneshi kama kuna mambo ambayo wewe na mwenzi wako mnafanana. Kama hamuendi sawa, jifunze kumuelewa.

Unaamini katika sanaa, mwenzako anadatishwa na michezo. Unapenda kusoma vitabu na kutoka kwenye matembezi ya hapa na pale, lakini yeye anapenda kusafiri. Hata hivyo, unapaswa kuamini kwamba ndoa ni kujitoa muhanga.

Siyo sawa na kutoa na kuchukua. Inatakiwa uwe mwelewa, katika kuhakikisha mapenzi yenu yanafanikiwa, ni vizuri ukahifadhi mambo yako kisha ukaungana naye kwenye mambo yake. Baadaye utamfanya aungane nawe kwako taratibu.

Hilo litafanikiwa kama utaacha ubinafsi. Tabia ya kutaka upendwe zaidi ni kosa. Katika uhusiano hutakiwi kujifikiria wa kwanza. Wekeza upendo mkubwa, halafu umfanye naye akupende. Si kwa haraka, bali taratibu.

Kama kila unaloamini wewe yeye yupo mbali, jifunze mambo yake kwanza. Muelewe kisha mshirikishe yako. Leo ukimfanya ajue kwamba unapenda kuogelea, keshokutwa mpe lingine na umjulishe kuwa ungependa mwende pamoja.

Itaendelea wiki ijayo.

Mapenzi bora hupitia katika mzani, jifunze kupima na kubalansi - 3

Kipengele cha jinsi unavyofanana na mwenzi wako ndicho kilitufungia sehemu ya nne ya makala haya. Naendelea kusisitiza kuwa haitakiwi kushindana, unapaswa kukubali kuachia vipaumbele vyako ili umpe nafasi mwenzi wako.

Ni mchezo mdogo lakini mgumu, maana yake ni kuyaweza mapenzi. Ni jambo ambalo lipo karibu na kutowezekana kwa mpenzi wa mpira kuacha ‘rimoti’ ya televisheni kwa mwenzi wake ili aangalie tamthiliya. Hata hivyo, endapo mtagombea rimoti, mwisho mtaanza kuchokana mapema.

KUNA MABADILIKO?

Vema kujiuliza swali hilo na matawi yake. Hii itakusaidia kutanzua mambo ambayo yanaweza kusababisha uhusiano wenu ukaenda na maji hapo baadaye.

* Kuna kiasi cha mabadiliko kwa kila mmoja wenu tangu mlipokutana kwa mara ya kwanza?

* Bado unachangia na mwenzi wako kila kitu chenu kama ambavyo mlifanya wakati mnaanza kupendana?

* Kinatokea nini pale kila mmoja hufanya mambo anayojisikia mwenyewe?

* Una muda kiasi gani kutumia na mwenzi wako? Je, unajihisi upo kwenye uhusiano imara na wenye mafanikio? Jiulize, inamaanisha nini kuwa na maslahi tofautin kati yako na mwenzi wako?

* Umewahi kutafakari na kugundua kwamba wewe na mwenzi wako, kila mmoja ni mtu huru lakini mmeamua kuwa pamoja au zipo dalili za kifungo?

* Je, unaamini mapenzi ni kujitoa mhanga? Kama ndivyo ni kwa nini?

JADILI MASWALI HAYO NA MWENZIO

Lazima maswali hayo uyapatie majibu, si kwa wewe peke yako bali kwa kushirikiana na mwenzi wako. Kama kuna sehemu yenye utata basi haraka sana, mnaitolea macho na kuondoa tofauti. Hakikisha kila kitu kinakuwa chanya.

Hata hivyo, pengine kila unapoweka mezani ‘ishu’ ya kujadili inageuka ubishi. Ndani ya ubongo wako, unaamua kuachana na ‘topiki’ hiyo kwa lengo la kuepuka migogoro. Unahisi mbele ya ubishi kuna ugomvi, nawe hupendi kugombana kwani inaweza kuhatarisha mapenzi yenu.

Hata hivyo, kuacha kujadili jambo ambalo linawatofautisha ni hatari zaidi, hivyo ni busara kutafuta meza ya mazungumzo kwa namna yoyote ile. Ni kosa kubwa kuwa na maslahi tofauti kwenye mapenzi. Mnaweza kutofautiana mambo mengine lakini siyo hilo.

Mathalan, wewe unaamini kwamba mpenzi uliyenaye kwake ndiyo umefika, yeye hilo halipo akilini. Unawaza ndoa mwenzako anakutafsiri kama ni wa kuzugia. Uhusiano wa namna hiyo haupo sawa, una matege, haufai kuendelea kujengwa. Unaweza kumrekebisha, kama habadiliki, ni bora ukimbie.

Vema ukajiuliza mwenyewe, ni muda gani utaishi na mtu ambaye hana mpango na wewe. Kila ukianzisha mada ya ndoa anakuwa mkali. Lazima wote muwe na maslahi ya aina moja, nyote mtamani kuoana, hapo mtaweza kufika, vinginevyo utakuwa unajenga, mwenzako anabomoa.

Kama nilivyotaka ujiulize hapo juu, kwamba wewe na mwenzi wako kila mmoja ni mtu huru. Hii inamaanisha kuwa mapenzi siyo kifungo. Unapaswa kumuacha aamue mwenyewe kuhusu hatma ya mapenzi yenu. Ukionekana unambana, anaweza kufanya mambo kukuridhisha lakini kuna siku atakuadhiri.

Baadaye anaweza kuthubutu kukwambia: “Sikutaka kufunga ndoa na wewe, sema tu ulinilazimisha.” Kauli hii ni tusi, endapo utaitafakari kwa mlengo kuwa uliyenaye hana mapenzi ya dhati nawe. Hata kuwa naye ni kama umemlazimisha.

Tafakari kisha upate jibu kwamba mwenzi wako hana hisia na wewe. Huo ndiyo ukweli kwa maana mapenzi ni hisia. Kama mwenzi wako anakupenda, maana yake ana hisia juu yako, baada ya hapo sasa tafsiri kinyume chake. Unaweza kujiona mdogo kama piritoni.

Hutakiwi kufika huko, vema ujiwekee utaratibu wa kutafakari kila hatua ya uhusiano wako. Kuna maswali mengi ambayo nimekutaka ujiulize. Hayo yatakusaidia kukupa picha ya uhusiano wako ulipo na unapoelekea.

Si kukimbiliia kuachana au kuvumilia yasiyovumilika kwa kudhani mwenzi wako atajirekebisha. Bila dira, hutafanikiwa. Vema ujue kuwa hakuna ugumu kwenye mapenzi kama utajifunza na kuyaelewa kikamilifu.

 
Tuesday, 19 March 2013 16:30 Al News - Love+Relationships
Print PDF

Inauma sana mchumba wako kuolewa na mwanaume mwingine

Brigitte ni mwaminifu kweli, alishaamua mapenzi yake kuyaweka kwa Abraham wake, kwa hiyo hata migogoro ilipokuwa inaibuka, yeye alivaa uvumilivu. Aliamini mume wake mtarajiwa ni binadamu, siyo malaika, hivyo alimeza upungufu wote aliomuona nao.

Kama kawaida, mwenye wivu haishiwi visa. Abraham akahakikisha anambana Brigitte kila upande. Mrembo akavumilia lakini mwisho akaanza kuona kero. Hakuwahi kusaliti penzi lao lakini akawa anatuhumiwa na kuitwa malaya.

Asiongee na mwanaume, kila rafiki yake wa kiume alituhumiwa anatembea naye. Abraham hakuishia hapo, akaanzisha tabia ya kuwatumia marafiki zake wamtongoze Brigitte, eti aone kama ni mwaminifu kweli au la!

Jerry, Gasper, Enock, Julius na Sulley, walishamtongoza Brigitte kama jaribio la Abraham kutaka kuona uaminifu wa mwenzi wake. Hakuna kati yao aliyefanikiwa. Wote walikumbana na majibu makavu kwamba wameshachelewa, kwani yeye ana wa kwake wanayependana sana.

Brigitte anapokutana na Abraham, humsimulia wanaume wote waliomtongoza na jinsi alivyowajibu. Siku alipotongozwa na Enock, hakusema. Hilo likawa kosa kubwa sana kwa Abraham ambaye alimtuhumu mwenzi wake kuwa alikuwa mbioni kumkubalia ndiyo maana ameficha ukweli.

“Huyu amejuaje kama nimetongozwa na yule kaka?” Brigitte alijiuliza bila kupata jibu, kisha akawaza akiumia: “Mimi nimemkatalia kabisa yule kaka, halafu Abraham ananimbia mimi nataka nimkubalie ndiyo maana sijasema.”

Siku moja akiwa kijiweni, Abraham alikuwa anamponda sana Brigitte kuwa ni mwanamke malaya. Gasper alimtolea uvivu, akampasha: “Tatizo kwenye miti mingi hakuna wajenzi. Yule Brigitte ni bonge la mwanamke, tena mwaminifu. Umeshatuma watu kibao wamchunguze wakamkuta yupo safi. Umetuma wanaume wamtongoze, wote wamekataliwa.”

Hamza anajua tatizo la Abraham ni wivu, hakuna asichokijua kuhusu Brigitte kwamba ni mwanamke mwaminifu, mstaarabu, mzuri na kadhalika. Hamza akamuuliza Abraham: “Unaonaje na mimi nikimtongoza, akikataa basi huyo ni wako peke yako, akinikubalia, basi hakufai.”

Abraham akakubali harakaharaka. Hamza akaingia kazini, akajitokeza kwa Brigitte kama mtu anayemhurumia kutokana na jinsi anavyotendwa na Abraham. Mwanzoni hawakuelewana kwa sababu Brigitte alisisitiza kwamba yeye na Abraham wapo vizuri sana.

Hamza hakuwa na haraka, aliendelea kuzungumza naye kama rafiki anayemtakia mema mpaka siku moja Brigitte akakubali wakutane, wale chakula cha jioni pamoja kisha wazungumze kwa ukaribu. Ni siku hiyo ambayo Hamza aliamua kumfungulia Brigitte kila kitu.

Alimweleza jinsi Abraham anavymponda na namna anavyotuma wanaume wamtongoze. Ni hapo ndipo Brigitte alipokumbuka ishu ya Enock, jinsi alivyomtongoza lakini akamkatalia, baadaye Abraham akamjia juu: “Kumbe alikuwa ananitega”

Hamza akafunguka: “Mwanamke mzuri kama wewe unatakiwa uwe na mwanaume makini, mwelewa, mtulivu kama mimi. Ukinikubalia tu, keshokutwa nakuja kwenu kutoa mahari. Sipo tayari kukupoteza.” Kwa nini Brigitte akatae? Siku mbili zilizofuata, Hamza na ujumbe wake, wakatinga nyumbani kwao Brigitte na kutoa mahari.

Siku tatu baadaye, Abraham alipokea simu kutoka kwa Hamza, akimtaka aende nyumbani kwake haraka, kwani ana siri nzito kuhusu Brigitte. Abraham akaenda haraka sana, alipofika alipokelewa na mdogo wa Hamza ambaye alimuongoza mpaka chumbani.

Ile kuingia tu, Abraham alishuhudia picha inayomuumiza mpaka leo. Aliwakuta Hamza na Brigitte kitandani katika pozi matata sana la mahaba. Alihamaki, akataka kupigana lakini Hamza akamwambia: “Wewe si ulimuona malaya ukawa humwamini? Sasa kafika kwanza, nilishamtolea mahari na mwezi ujao namuoa.”

Abraham alianguka kama mzigo, fahamu zilipomrudia bado hakuweza kubadili matokeo. Mwezi mmoja baadaye, Hamza na Brigitte walifunga ndoa. Ikamuuma sana, kwani huyo aliyeolewa ndiye aliota kumuoa lakini amepigwa bao. Inamuuma mchumba wake kuolewa na mwanaume mwingine lakini hana cha kufanya.

 

 

Page 1 of 24

<< Start < Prev 1 2 3 4 5 6 7 8 9 10 Next > End >>